.

.
Thursday, September 26, 2013

4:20 AM

WAZIRI wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe ametakiwa ajiuzulu kwa kutoa taarifa za uongo kwamba Zanzibar ilishirikishwa kabla ya Muswada wa Mabadiliko ya Katiba kuwasilish
wa bungeni na kupitishwa na Bunge Septemba mwaka huu.
Msimamo huo ulitolewa na Waziri wa Sheria na Katiba Zanzibar, Aboubakary Khamis Bakari wakati akihutubia mkutano wa hadhara uliovishirikishwa vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi uliofanyika Uwanja wa Kibandamaiti mjini Unguja jana.
Aboubakari alisema kwamba Zanzibar ilipokea taarifa ya awali ya mabadiliko kuhusu vifungu vinne vya Muswada wa Mabadiliko ya Katiba na kutakiwa Zanzibar itoe maoni na mapendekezo yake, jambo ambalo alisema lilifanyika kupitia Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Hata hivyo, alisema vifungu vya mabadiliko ghafla viliongezwa kutoka vinne hadi 12 bila ya Zanzibar kupewa nafasi ya kujadili vifungu vinane ambavyo vina umuhimu mkubwa katika kupata katiba bora.
“Waziri nimesoma naye Chuo Kikuu mwaka 1972, Chikawe kwa hili amesema uongo vinginevyo ajiuzulu, hafai,” alisema Aboubakari.
Alisema kabla ya kufanyika Waziri akifuatana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Bunge, William Lukuvi walifika Zanzibar na kutaka wajadili vifungu hivyo kwa siku moja jambo ambalo alipinga kulitekeleza.
“Baada ya kuanza kupiga kelele, wenzetu walikuja Zanzibar wakitaka tujadili mabadiliko ya mswada,nikawaambia siwezi kujadili masilahi ya nchi kijuujuu, huko ni kuiuza nchi, siko tayari kufanya hilo,” alisema.
Aboubakari alisema marekebisho yaliyofanyika katika muswada huo na kutoa nafasi kujadili na kupitisha mabadiliko ya Katiba kwa kutumia wingi wa kura ni sawa na wazimu.
Alisema mabadiliko yoyote ya Katiba yanapaswa kutumia theluthi mbili toka pande mbili za Muungano, utaratibu ambao ndiyo umekuwa ukitumika na nchi mbalimbali zenye mfumo kama wa Tanzania. 

Mwananchi ilipomtafuta Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe kujibu tuhuma hizo alisema Aboubakari ameudanganya umma mchana kweupe kwa vile yeye na Waziri Lukuvi walifika Zanzibar kupeleka rasimu ya muswada na si kujadili na kupokea mapendekezo papo kwa hapo.
Chikawe alisema kwamba walipokabidhi muswada pia walimtaarifu siku ya kuwasilishwa muswada huo katika kikao cha Bunge na kuwataka kutoa maoni na mapendekezo kwa wakati mwafaka kabla ya kujadiliwa na kamati ya Katiba ya Sheria ya Bunge.
Alisema kwamba nyongeza ya marekebisho ya vifungu vinane yalitokana na mapendekezo ya wabunge katika kamati na michango ya wabunge ndani ya Bunge katika utaratibu unaoruhusiwa kisheria.
“Baada ya kamati ya Bunge kukaa, Mbunge Halima Mdee wa Chadema ndiye aliyependekeza kutumika kwa utaratibu wa wingi wa kura katika kupitisha mabadiliko hayo ya Katiba kama hatua ya theluthi mbili itashindwa kufikia mwafaka,” alisema Chikawe.
MWANANCHI

0 comments:

Post a Comment