.

.
Monday, June 9, 2014

11:32 PM
Rais Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwasili Dodoma keshokutwa, ikiwa ni siku moja kabla ya kuwasilishwa kwa Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2014/15.

Habari zilizopatikana jana zinasema Rais ataongoza kikao cha Baraza la Mawaziri kitakachopewa muhtasari kuhusu Bajeti ya Serikali ya mwaka ujao wa fedha na baadaye atafuatilia uwasilishaji wa bajeti hiyo bungeni akiwa Dodoma.

Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salva Rweyemamu alisema asingeweza kuzungumzia suala hilo kwa kuwa yuko likizo lakini akaweka bayana kwamba kwa kawaida kabla ya bajeti kuwasilishwa bungeni, lazima Baraza la Mawaziri lipewe muhtasari wa bajeti husika.

“Ni kawaida kabla ya bajeti kuwasilishwa, Rais huongoza kikao cha Baraza la Mawaziri yaani pre budget cabinet meeting ambako Waziri wa Fedha hutoa briefing (muhtasari) kuhusu maeneo muhimu ya bajeti, kwa hiyo siyo jambo jipya ni suala la kawaida,” alisema Rweyemamu.

Itakumbukwa kuwa mwaka jana kabla ya kusomwa kwa bajeti ya 2013/14, Rais Kikwete alikuwa Dodoma ambako pamoja na kukutana na mawaziri, pia alifanya kikao na Kamati ya Bunge ya Bajeti.

Hata hivyo, uwepo wake mjini Dodoma safari hii umekuja wakati kukiwa na dalili za mvutano mkubwa kati ya Bunge na Serikali kutokana na kutotolewa kwa fedha za kutosha za maendeleo kwa mwaka wa fedha unaoisha Juni 30 mwaka huu.

Taarifa zinasema bajeti inayomalizika mwishoni mwa mwaka huu, inapungukiwa kiasi cha Sh1.8 trilioni, huku Serikali ikilaumiwa na wabunge kwa kutoa misamaha ya kodi inayofikia Sh1.52 trilioni, ambayo ingepunguza nakisi iliyopo kwenye bajeti kwa asilimia 84.4.

Wakati wa mjadala wa bajeti za wizara tangu kuanza kwa Bunge la Bajeti Mei 6 mwaka huu, wabunge wamesikika mara kadhaa wakilalamika kwamba fedha za maendeleo zilizotolewa kwa wizara katika bajeti ya 2013/14 ni kati ya asilimia 25 na 30, jambo ambalo limesababisha kukwama kwa miradi mingi.

Keshokutwa itakuwa siku ya mwisho ya mashauriano baina ya Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Bunge kupitia Kamati yake ya Bajeti inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge.

Mazungumzo hayo yaliyoanza Juni 5 mwaka huu, yalilenga kuangalia uwezekano wa kutafuta vyanzo vipya vya mapato ili kuwezesha kuzingatiwa kwa ushauri wa wabunge, pamoja na kusaka fedha kuziba pengo la Sh1.8 trilioni katika bajeti ya 2013/14.

Alipoulizwa jana, Chenge hakuwa tayari kuzungumzia hatua iliyofikiwa katika mashauriano hayo na badala yake alisema kwa ufupi: “Ndugu yangu mambo ya Bunge, tutakutana kwenye taarifa yetu ya kamati tutakayoiwasilisha bungeni.”

0 comments:

Post a Comment