.

.
Friday, September 19, 2014

10:03 AM

MUENDELEZO wa Jeshi la Polisi nchini kuwanyanyasa, kuwatisha waandishi wa habari na kuwafanya wasitekeleze wajibu wao ipasavyo, ilijidhihirisha wazi jana makao makuu ya jeshi hilo, baada ya waandishi kupigwa, kukimbizwa na mbwa ili wasichukue taarifa za kuhojiwa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe.

Tukio la kupigwa na kudhalilishwa kwa waandishi wa habari lilitokea jana, limetokea ikiwa ni siku moja baada ya Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal, kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama nchini kushirikiana na waandishi wa habari katika kufanya kazi kwa ajili ya kulinda amani ya nchi.

Waandishi waliyopigwa na Polisi hiyo jana ni Josephat Isango anayeandikia gazeti hili, huku Yusuph Badi ambaye ni mpiga picha wa magazeti ya serikali, akipigwa na ‘kusakiziwa’ mbwa ili wamuume.

Dalili za waandishi wa habari kuzuiwa kufanya kazi yao, zilianza kujionesha mapema jana wakati Mbowe alipowasili katika makao makuu ya Jeshi la Polisi, ambako waandishi walizuiwa wasiingie katika eneo hilo kwa ajili ya kuchukua picha na maelezo ya kiongozi huyo.

Akiwa anawaongoza askari wake katika amri ya kushambuliwa kwa waandishi wa habari hiyo jana, Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja, alisikika mara kwa mara akiwaagiza vijana wake wawaondoe waandishi na hata kuwasakizia mbwa.

Chagonja, alisikika mara kadhaa akitoa amri kwa askari kuwa wawafungulie mbwa ili waweze kujeruhi angalau mtu mmoja kutoa funzo ili wafuasi wa CHADEMA waliokuwa kwenye lango kumsubiri Mbowe waondoke.

“Waondoeni wote msiwaruhusu hata hao waandishi kuingia humu, ninyi askari wa mbwa mnafanya nini hapo wakati watu wamejazana mlangoni wapelekeeni hao,” alisikika akisema Kamishna Chagonja.

Mara baada ya maelekezo hayo ya Kamishna Chagonja, askari waliokuwa na mbwa walianza kuwakimbiza wafuasi wa CHADEMA na waandishi wa habari.

Katika hali ya kustaajabisha, askari watatu kwa pamoja walimfuata Josephat Isango, aliyekuwa akitoka katika lango kuu na kuanza kumshambulia kwa rungu na mateke hali iliyowafanya waandishi wa habari kuingilia kati kwa ajili ya kumnusuru.

Baada ya waandishi kumnusuru Isango, kipigo kiligeukia kwa Mwandishi Yusuph Badi, ambaye wakati akishambuliwa alianguka chini huku askari wenye mbwa wakiwaachia kwa ajili ya kumshambulia.

Kilichomnusuru Badi asiumwe na mbwa hao ni kamera aliyoishika mkononi na kujikinga ili asidhurike, kitendo hicho cha kujikinga kilisababisha kuharibika kwa kifaa hicho.

Wakizungumza baada ya hali kutulia, Badi na Isango, walieleza kuwa kilichofanywa na jeshi la Polisi ni kuminya uhuru wa utendaji kazi wa waandishi katika kuuhabarisha umma wa watanzania juu ya mambo yaliyokuwa yakitokea.

“Ni jana tu wameambiwa namna ya kutoa ushirikiano na vyombo vya habari, lakini leo wanatupiga na kutusakizia mbwa hii si haki na viongozi wetu wanapaswa waangalie mara mbili mbili namna ya kushirikiana na jeshi hili,” alisema Badi.

Jeshi la Polisi limekuwa na kawaida ya kuwanyanyasa, kuwapiga na hata kuwaua waandishi wa habari pale wanapotekeleza wajibu wao wa kukusanya habari.

Tukio linalokumbukwa zaidi la ukatili wa askari wa jeshi hilo kwa waandishi wa habari ni mauaji ya Mwandishi wa kituo cha Televisheni ya Chanel ten mkoani Iringa, Daudi Mwangosi, mauaji yaliyotokea Septemba 2 mwaka juzi katika Kijiji cha Nyololo Mufindi mkoani Iringa wakati mwandishi huyo akiwajibika

0 comments:

Post a Comment