.

.
Friday, November 28, 2014

2:47 AM
Watu wengi wamekuwa na shauku ya kutaka kujua ugonjwa wa saratani ya tezi dume, huku wakidhani ni mpya. Lakini ukweli ni kuwa umekuwapo miaka mingi na wengi wameugua.
Takwimu zinaonyesha wanaume wengi huugua ugonjwa huu unaoongezeka kwa kasi ya hali ya juu.
Kulingana na utafiti uliofanywa na Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORIC), kutoka mwaka 2006, zinaonyesha kuwa kila mwaka kumekuwa na ongezeko la kesi mpya ya wagonjwa saratani ya tezi dume.
Novemba ya kila mwaka, jumuiya za kimataifa huadhimisha tukio ambalo hujulikana kama Movemba.
Maadhimisho hayo huhusisha kukuza kwa masharubu, kukusanya fedha na kuleta mwamko na ufahamu wa masuala ya afya kwa wanaume kama vile saratani ya tezi dume.
Jina hilo la Movemba ni mchanganyiko wa neno ‘Masharubu na Novemba’.
Maadhimisho hayo ya mwezi mzima yanalenga kuongeza ufahamu na mwamko kwa kupima ili kugundua mapema.
Mwaka jana peke yake zaidi ya Dola za Marekani 120 milioni zilikusanywa.
Hadi sasa, Movemba imekusanya zaidi ya Dola 550 milioni kupitia wanachama wake milioni nne katika nchi 21 duniani kote.
Waziri mstaafu wa Afya na Ustawi wa Jamii, Profesa David Mwakyusa alinukuliwa akisema asilimia 10 ya wagonjwa wanaosumbuliwa na aina mbalimbali za saratani wamejitokeza hospitalini kwa uchunguzi na matibabu.
Anasema asilimia 90 iliyobaki hawajafanya jitihada zozote kuhudhuria uchunguzi na matibabu.
Akizungumzia juu ya uchunguzi wa hali ya tezi dume nchini, Mwanzilishi na Mwenyekiti wa Hospitali ya Apollo yenye makao makuu India, Dk Prathap Reddy anasema kuwa ugonjwa huo unaathiri watu wengi na kusababisha vifo vingi nchini kwa sababu ya ukosefu wa ufahamu wa kina juu ya ugonjwa huo.

0 comments:

Post a Comment