WAANDISHI wawili wa habari wa Kampuni ya New Habari (2006),
wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha wakikabiliwa na kosa
la kupokea rushwa ya sh.150,000 kutoka kwa mmiliki na Chuo cha Savana
Bridge, kilichopo jijini hapa.
Waandishi hao, Isack Longwe (28) mkazi wa Tegeta, Tanki bovu na Fredy
Okoth (36) mkazi wa Kimanga Tabata jijini Dar es Salaam, wanadaiwa
kushawishi kupatiwa sh. laki tatu ili waharakishe usajili wa chuo hicho
kwenye Baraza la Taifa la Vyuo vya Ufundi (Nacte).
Walifikishwa mahakamani jana na kusomewa mashtaka mawili ya
kushawishi na kupokea rushwa na Mwanasheria wa Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru), Vailet Machali mbele ya Hakimu
Mkazi, Rose Ngoka.
Alidai kuwa washtakiwa hao walikamatwa Agosti 16 mwaka huu mchana,
baada ya kupokea kiasi hicho cha fedha ikiwa ni sehemu ya sh. 300,000
walizokuwa wameshawishi kupatiwa.
Akiwasomea maelezo ya kosa, Ngoka aliieleza mahakama hiyo kuwa
washtakiwa wote kwa pamoja mnamo Agosti 14 mwaka huu, wakiwa Jiji la
Arusha walimshawishi mmiliki ambaye pia ni Mkuu wa chuo hicho, Mselemu
Kombe kuwapatia sh. 300,000, ili wakaharakishe usajili wake Nacte.
Katika shtaka la pili, washtakiwa hao walidaiwa kuwa Agosti 16 mwaka
huu, majira ya mchana, walipokea rushwa ya sh.150,000 toka kwa Mselemu
kwa lengo hilohilo.
Ngoka alidai kuwa washitakiwa hao walifanya makosa hayo huku wakijua
wao kama waandishi wa habari hawawezi kufanya shughuli za usajili wa
chuo.
Hadi Tanzania Daima linaondoka mahakamani hapo, waandishi hao
walikuwa rumande ya mahakamani hapo wakisubiri kupata wadhamini wawili
wenye vitambulisho na mali isiyohamishika yenye thamani ya sh. milioni
moja, vinginevyo wangepelekwa gereza la Kisongo hadi Septemba 2, mwaka
huu, shauri hilo litakaporudi kwa ajili ya kutajwa.
chanzo tz daima
Home
»
»Unlabelled
» Waandishi kortini kwa rushwa
Wednesday, August 20, 2014
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment