.

.
Tuesday, July 28, 2015

7:12 AM



Bertha Ismail

Arusha . Pamoja na kuwa chama cha mapinduzi imekamilisha zoezi la kumpata mgombea Urais wa chama hicho mwezi Octoba mwaka huu lakini Dhambi ya  kumkata  aliyekuwa  mmoja wa wagombea Urais Edward Ngoyai Lowassa imeendelea  kukitafuna chama hicho baada ya mwenyekiti mkoa wa Arusha Onesmo Ole Nangole kuonyesha wazi kuumizwa na matokeo hayo.

 Hali hiyo imejitokeza jana mkutano maalumu  wa uchaguzi wa wabunge viti maalumu kupitia Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) uliofanyika  katika ukumbi wa mikutano wa AICC mjini hapa ambao ulihudhuriwa na wajumbe kutoka wilaya zote za mkoa wa Arusha ambazo ni Longido, Ngorongoro, Karatu, Arumeru, Arusha mjini na Monduli.

Nangole alisema kuwa pamoja na kamati kuu ya CCM kumpitisha Dr. Magufuli lakini uchaguzi huo haukuwa wa haki na usawa kwani hata Lowassa alikuwa na sifa zote za kupitishwa kwenye hatua za awali lakini alikatwa jambo ambalo limewaumiza sana na hadi leo wana Arusha wanaumwa kutokana na haki haikutendeka pamoja na kujitokeza kunyosha mkono kutoa hoja kwenye mkutano huo lakini walizuiliwa

“Naomba niseme kwa hili CCM iliyofanya imesababisha chama chetu kuingia kwenye hali ya chuki na kuendesha mapambano ya sisi kwa sisi badala ya mapambano hayo kuelekeza upinzani hali ilipelekea baadhi yetu kuchukua maamuzi magumu ya kuhama chama na kusaliti ,.. na kutokana na hili chama chetu hakitafika mbali kama watakuwa wanawafanyia hivi watu wenye sifa, na ijulikane kuwa chama hiki ni cha watu wote hivyo tusijione wengine wakubwa na kuwadharau wengine kwa kutumia vyeo vyetu kuwadhalilisha”

  “Ndugu zangu baadhi yenu hamkuwepo kwenye huu uchaguzi hivyo niwaambie wazi kuwa Lowasa alionewa kwani sifa za kamati ya maadili kumpitisha lakini kutokana na chuki binafsi bila kujali ni chaguo la wananchi wengi wanamkubali wakamkata” alisema Mwenyekiti Ole Nangolo ambae alishangiliwa mda wote kuonyesha maneno hayo yanawagusa wajumbe.


Nangole akizungumza kuhusiana na uchaguzi huo wa UWT, aliwataka
wanawake kufanya maamuzi sahihi ya kuwachagua viongozi wenye uchungu na mapenzi mema na wanawake hao ambao watakuwa tayari wakati wowote kubeba matatizo yao.

Aliwataka wanawake hao kuchagua  viongozi  ambao  watakuwa tayari
kufika katika maeneo ya wananchi kusikiliza kero zao na kuzipatia
ufumbuzi na sio viongozi wanaofika kwa mwaka mara moja pindi
wanapohitaji  kura .

‘kila mmoja anajua kuwa kazi ya mbunge ni kushughulikia kero za
wananchi usiku na mchana na sio kuwafuata wananchi kwa msimu  na nyie wenyewe mnawafahamu vizuri msifanye makosa katika uchaguzi huu chagueni kiongozi kwa manufaa yenu wenyewe ‘alisisitiza Nangole.

Naye Katibu  wa UWT Mkoa wa Arusha, Fatuma Hassan aliwataka wanawake hao kuhakikisha wanawachagua viongozi wanaojali maslahi ya wananchi hususani wanawake  kwani hivi sasa ndipo wanapotakiwa kufanya maamuzi yaliyo sahihi.

Aliwataka  wanawake hao kuwa  makini katika kuwachagua viongozi wenye kujali shida na changamoto za wananchi na watakaokuwa tayari kuleta maendeleo kwa wakazi wa jiji la Arusha na wasikubali kurubuniwa na mtu yeyote bali maamuzi wafanye wao wenyewe.

Kwa upande wake msimamizi wa Uchaguzi huo ambae ni mkuu wa mkoa wa Arusha Daudi Filex  Ntibenda alisema kuwa endapo wajumbe hao watafanya makosa ya kumchagua mtu asiyekubalika basi wasilalamike kuwa hawana maendeleo bali wawalaumu waliompa dhamana.

Mwisho.

0 comments:

Post a Comment