.

.
Thursday, October 31, 2013

1:15 AM
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjJ26H5Kj6oZ0nPm_s5cQBGSv2AwS9ZVW__gTfeQoBMIf496Apw4TwrFtPD83H9k75wAF4WKXYCcaWlzy6Nxj2D0OMQp49Ujx87X2f9fUK9duUuY9hXKKmzqW0C6ZIiwWtGOl8INzcoHkTw/s400/Samwel_Sitta.jpgWAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, amesema Tanzania itatoa talaka kwa nchi za Rwanda, Kenya na Uganda ambazo zimeamua kuanzisha Jumuiya ya hiari nje ya Jumuiya ya Afrik
a Mashariki.


Sitta alisema kutokana na nchi hizo kuonekana kuitenga Tanzania na Burundi ambazo ni wanachama wa jumuiya hiyo, wameshaanza mazungumzo ya kushirikiana kiuchumi, kisiasa na nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Congo (DRC).


Kauli hiyo ya Sitta inatokana na mikutano ya mara kwa mara inayofanywa na marais Uhuru Kenyata wa Kenya, Paul Kagame (Rwanda) na Yoweri Museveni (Uganda) kuzungumzia masuala mbalimbali ya kushirikiana nje ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Waziri Sitta alibainisha msimamo wa Tanzania kutengwa na nchi hizo tatu jana bungeni, alipokuwa akijibu maswali ya wabunge mbalimbali waliokuwa wakitaka kujua kauli ya serikali juu ya vikao vinavyofanywa na marais hao watatu.


Mbunge wa Viti Maalumu Rukia Ahmed (CCM), aliitaka serikali ipeleke pendekezo bungeni la kujitoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kabla haijapewa talaka kutoka kwa Rwanda, Uganda na Kenya ambazo zimekuwa zikifanya mikutano inayojadili masuala ya jumuiya bila kuihusisha serikali ya Tanzania.


Akijibu hoja hiyo Sitta, alisema ni mapema kwa Tanzania kupeleka bungeni hoja ya kujitoa katika jumuiya hiyo kwa kuwa kinachofanywa na nchi hizo kimeshafikishwa kwa Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa nchi wanachama ambaye atakitolea ufafanuzi katika kikao kitakachofanyika wiki mbili zijazo.


Sitta alifafanua kauli ya Waziri mwenzake wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, hivi karibuni ya kwamba Tanzania inasubiri talaka akisema yenyewe ndiyo yenye uwezo wa kutoa talaka kwa jumuiya hiyo kwa kuwa inamiliki asilimia 52 ya eneo lote huku nchi zilizobakia zikigawana asilimia 48 iliyobakia.


“Hawa wenzetu wanafanya utoto wa kutuzunguka, sisi tunatumia hekima za mzee Mwinyi aliyesema ‘mwongo, mwongoze’. Kama wao wana hila zozote juu yetu, siku si nyingi tutazibaini, kama ni ndoa kwenye jumuiya basi sisi ndio tutakuwa tumeoa…hivyo tutatoa talaka wakati wowote,” alisema.


Naye Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela (CCM), aliitaka serikali isiendelee na hatua zozote kwenye jumuiya hiyo ambayo inaonekana kuelekea kuvunjika.


Akijibu swali hilo, Sitta alisema serikali haijakaa kimya bali imeamua kutoshiriki vikao vyote ambavyo nchi za Kenya, Rwanda na Uganda zitakuwa zimeshayazungumzia masuala husika na kuamua kuwa na msimamo wa pamoja nje ya jumuiya.


Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), alihoji serikali inangoja utafiti gani juu ya kutengwa kwao kiuchumi na nchi hizo tatu wakati Kenya wameshaingia makubaliano ya kibiashara na Ethiopia na Sudan.


Katika jibu lake, Sitta alisema Tanzania imeshafanya mazungumzo na nchi za DRC na Burundi kushirikiana katika nyanja mbalimbali.
Alisema kuwa DRC ndiyo yenye manufaa makubwa kiuchumi kwa Tanzania kuliko Rwanda, Uganda, Kenya na Burundi kwa sababu mizigo mingi hutegemea bandari ya Dar es Salaam.


“Burundi nao wanatengwa kama tunavyofanyiwa sisi, lakini tumeamua kushirikiana kikamilifu na DRC pamoja na Burundi ambao tuna imani wana manufaa makubwa kwetu,” alisema.


Hivi karibuni Tanzania iliingia kwenye mgogoro na Rwanda baada ya Rais Jakaya Kikwete kutoa ushauri kwa Rais wa Rwanda, Kagame kuketi chini na waasi wa nchi hiyo ili kuzungumzia masuala ya amani kwa nchi yao. TANZANIA DAIMA

0 comments:

Post a Comment