.

.
Wednesday, July 24, 2013

10:03 AM
 
Chadema kimepinga kauli ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba kuhusu hatima ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 kikisema mchakato wa sasa wa Mabaraza ya Katiba, usiwe kikwazo cha mjadala wa muundo wa Serikali Tatu.
Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Chadema, John Mnyika alisema Dar es Salaam jana kuwa hatima ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 utakaotokana na mchakato wa mabadiliko ya Katiba unaoendelea, siyo suala la kusubiri.
Akizungumza na mwandishi wetu juzi kuhusu kauli ya Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe kwamba endapo mapendekezo ya Serikali Tatu yatapitishwa, kuna hatihati ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 kufanyika, Jaji Warioba alisema: “Tuachieni muda… hayo mengine ni hisia tu. Ni kweli tunayajua lakini acheni tumalize hili kwanza ( la Mabaraza ya Katiba). Hii ndiyo hatua tuliyopo sasa.”
Lakini jana Mnyika alisema: “Hatuwezi kusubiri hadi Mabaraza ya Katiba yakamilishe mchakato kama alivyoeleza Jaji Warioba katika gazeti lenu la Mwananchi toleo la leo, (jana),” alisema Mnyika kwa simu.
Jaji Warioba alitaka suala la muundo wa Serikali Tatu utakavyokuwa lisiwe hoja kwa sasa kwa kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba inachokifanya ni kukusanya maoni kupitia Mabaraza ya Katiba na kisha kuandaa rasimu itakayopelekwa bungeni kwa ajili ya majadiliano na kwamba mjadala huo utawachanganya wananchi endapo utaingizwa katika hatua hii ya ukusanyaji maoni.
Lakini Mnyika alisema: “Mijadala hii haiwezi kusubiri mpaka hatua ya Mabaraza ya Katiba, inapaswa kuanza wakati huu kupitia mabaraza yanayosimamiwa na Tume na Mabaraza yanayoendeshwa na makundi ya kijamii. “Pia, masuala hayo ya mpito pamoja na marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, ni mambo ambayo yanapaswa  kutolewa ufafanuzi wa ziada na Serikali zaidi ya kauli ambayo Waziri wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe ameitoa kupitia gazeti la lenu la leo (jana).”
Alisema kimsingi bado kunahitajika mjadala wa masuala ya mpito kwa sababu kuna uwezekano kwamba Katiba Mpya, ya Muungano au ya Zanzibar na ya Tanganyika, isiwe tayari kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, endapo suala la Serikali tatu litapita.
Alisema kwa upande mwingine, rasimu ya Katiba iliyotolewa imeibua mjadala juu ya mkwamo wa kikatiba (constitutional stalemate), ambao ni muhimu upatiwe suluhisho akisema chama chake kinapendekeza mchakato wa Katiba Mpya ya Tanganyika uanze mara moja ili uende sambamba na huu wa Katiba Mpya ya Muungano. Alisema ilikuwa vyema yote yakajadiliwa katika Bunge la Agosti 27, mwaka huu.
Waziri Chikawe alikaririwa na gazeti hili juzi akisema: “Uwepo wa Serikali tatu utafumua mfumo mzima wa utendaji ndani ya Serikali. Hatuwezi tena kufanya uchaguzi wa Rais na wabunge 2015, hatuwezi kufanya chochote nje ya Katiba ya Serikali Tatu kwa kuwa kinachofuata ni kuunda Katiba nyingine inayohusiana na Serikali tatu.
Waziri Chikawe afafanua
Juzi, Waziri Chikawe alitoa ufafanuzi juu ya utata wa hoja zake kwa kuipongeza Tume ya Jaji Warioba kwa kazi inayofanya huku akisema anaunga mkono msimamo wa CCM wa kutaka kuendelea na muundo wa Muungano wa Serikali mbili.


Alisema mchakato wa kuandika Katiba Mpya unapaswa kuangaliwa kwa jicho pana zaidi ya lile la Uchaguzi Mkuu wa 2015.

0 comments:

Post a Comment