.

.
Thursday, March 26, 2015

5:35 AM
Arusha

Wadau wa michezo mkoani Arusha wamemtaka Naibu Waziri wa Vijana Utamaduni na Michezo atembelee na kukagua uwanja wa Sheikh Amri Abeid ajionee jinsi ulivyo katika hali mbaya kiasi cha kutokuwa katika hadhi ya kuchezewa hata mashindano ya mchangani.

Kauli ya wadau imekuja baada ya Naibu Waziri Juma Mkamia kutoa kauli kuwa uwanja wa Sheikh Amri Abeid ni katika viwanja bora vinavyotambulika na shirikisho la mpira Afrika (CAF) na unaweza kutumika na michezo ya kimataifa, kauli iliyopingwa vikali.


Viongozi wa vilabu, wachezaji na hata wadau wa soka wameshangazwa na kauli ya Mkamia na kuonyesha wasiwasi kuwa Waziri huyo hajawahi kuutembelea na kuujuwa vema uwanja huo  kwa kuukagua uwanja na miundo mbinu yake.                                                          

Eliapenda Zambia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya michezo ya TACODA alisema kuwa hali ya uwanja ni mbaya mno kiasi kwamba ni bora kucheza katika viwanja vya mchangani kuliko uwanja wa Sheikh Amri Abeid uliotawaliwa na mashimo, vichuguu, milima na mabonde huku vyoo vikiwa tatizo.

Juu ya miundombinu ya uwanja huo pamoja na uwepo na maji ya kutosha lakini hakuna vyoo vya watazamaji na vya wachezaji vikiwa vichafu na kuweka hali ya ukungu huku baadhi ya vyumba vya choo vikigeuzwa maduka na kupangisha wafanyabiashara na kuwa sehemu ya mapato ya CCM wenye uwanja.                                                                                            
Aidha suala hilo liliwahi kupigiwa kelele na wasimamizi wa vituo vya  ligi ya Vodacom, Daraja la kwanza na viongozi wa chama cha mpira mkoa (ARFA) juu ya kurekebisha vyumba vya kuvalia wachezaji pamoja na vyoo kuweka marumaru na madirisha lakini jitihada hizo hazijazaa matunda mpaka sasa huku nyasi zikikauka kabisa na kujenga hali ya viraka.

Waziri Juma Mkamia ameingia katika tuhuma hizo baada ya kutoa majibu yenye ukakasi bungeni alipotakiwa kutoa ufafanuzi juu ya vilabu kuwa na viwanja vyake na jitihada ya serikali kuboresha viwanja vya michezo hapa nchini.

Kwa upande wake Katibu wa chama cha soka mkoa wa Arusha alisema kuwa jiografia ya uwanja huo ni nzuri ila mapungufu machache yanayoukabili uwanja huo ikiwemo sakafu ya vyumba vya kubadirishia nguo wachezaji na uhaba wa vyoo vya watazamaji.

“Ni kweli uwanja huo una mapungufu hayo ila tumeshaongea na meneja wa uwanja kuufanyia marekebisho uwanja huo kwa mujibu wa maagizo ya TFF yaliyotolewa na raisi wa TFF Jamal Malinzi mwishoni mwa mwaka jana”

Meneja wa uwanja huo Andrew Mneja alisema kuwa tiyari mikakati ya kuuboresha uwanja huo unafanyika ambapo wataufunga wiki ijayo march 25 na tiyari wakandarasi wameshakagua na wataanza maboresho karibuni ikiwemo kuumwagilia kustawisha nyasi.

Mwisho………….

0 comments:

Post a Comment