.

.
Thursday, April 17, 2014

10:40 PM


MATUMAINI ya kumpata mshitakiwa namba moja katika kesi ya kusafirisha wanyama hai wakiwamo twiga wanne kwenda nchini Qatar, Kamran Ahmed, yameyeyuka baada ya jana mshitakiwa huyo kutofika tena mahakamani.
Mshitakiwa huyo amekuwa hafiki  mahakamani  kwa mara ya nne sasa huku kukiwa hakuna taarifa rasmi za kutofika kwake kutoka kwa wadhamini wake wala wakili wake, Edmund Ngemela.
Kesi hiyo ilikuja kwa kutajwa jana mbele ya Hakimu Mkazi, Simon Kobelo, anayesikiliza shauri hilo na baada ya mshitakiwa huyo kushindwa kufika mahakamani.
Mahakama imepanga kuanza kusikiliza kesi hiyo mfululizo Mei 6 na 7 mwaka huu.
Wakili wa Serikali, Patrick Mwita, aliiambia mahakama jana kuwa mshitakiwa huyo hakufika mahakamani na kusisitiza hati ya kukamatwa iendelee kuwa pale pale kama ilivyoamuliwa na mahakama.
Tayari upande wa mashitaka umeanza kufuatilia anwani za wadhamini wa mshitakiwa huyo, ili wakamatwe kutokana na kutofika mahakamani kutoa taarifa juu ya mshitakiwa huyo kama masharti ya dhamana yanavyoagiza.
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Hawa Mang’unyuka, Martin Kimath na Michael Mrutu ambao wote wako nje kwa dhamana.
Washitakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kusafirisha wanyama hao hai Novemba 26, mwaka 2010 kwenda Qatar kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), wanyama wanaodaiwa kukamatwa maeneo ya Mto wa Mbu, Elboret na Engaruka wilayani Monduli, mkoani Arusha.
Wanyama hao wenye thamani ya sh milioni 170.5 wanadaiwa kusafrishwa kwenye maboksi marefu ndani ya ndege kubwa ya jeshi la Qatar.

0 comments:

Post a Comment