.

.
Monday, November 18, 2013

10:06 PM

 
Junior Msenga akipatiwa huduma ya kwanza na daktari baada ya kupata ajali kufuatia gari waliokuwa wakisafiria aina ya Noah kugongana na lori eneo la Wami-Sokoine barabara kuu ya Dodoma-Morogoro wakati wakitoka katika mji mdogo wa Gairo kuelekea Morogoro mjini iliyotokea majira ya alfajili ya 11:45 mkoani Morogoro leo.



NA MTANDA BLOG.
MAITI sita kati ya saba ya ajali iliyohusisha gari ndogo aina ya Noah na lori, katika eneo la Dakawa Ranchi, Wami Sokoine, katika barabara kuu ya Morogoro-Dodoma, wametambuliwa.


Akizungumza na waandishi wa habari ofsini kwake, Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, amewataja waliofariki kwenye ajali hiyo kuwa ni pamoja na Isack Mehele (25) mfanyakazi wa kiwanda cha Tumbaku cha ALLIANCE ONE  na mkazi wa Manispaa ya Morogoro, Sam Elisha (40), ambaye ni Daktari wa Mimea, Maugo Salum (30), Sophia Hassan (20), Adini Mwisholwa (70) wote wakazi wa Gairo, na mwanaume mmoja ambaye jina lake halijaweza kufahamika mara moja.

Ajali hiyo imetokea leo Novemba 18 mwaka huu, majira ya  saa 11 :45 baada ya magari hayo mawili ikiwemo Noah iliyokuwa ikiendeshwa na Masoud Omary (28) mkazi wa Kihonda Manispaa ya Morogoro ambaye ni miongoni mwa waliopoteza maisha, kugongana uso kwa uso na Lori aina ya Scania  lililokuwa likiendeshwa na Musa Lukale (62) mkazi wa Mkoani Tabora.

Majeruhi wa ajali hiyo wametambuliwa kuwa ni Juma Mohamed (21) mkazi wa Gairo,  Hashim Ally Dafa (42) mkazi wa Lushoto, Junior Msenga, Selemani Hamis (20) mkazi wa Babati Manyara, Martin Msobi, mkazi wa Dumila, Festo Paulo mkazi wa Kimara mwisho jijini Dar es salaam na mwimgine mmoja ambaye jina lake halijaweza kutambuliwa mara moja kutokana na kuwa katika hali mbaya.

Daktari Bingwa wa Upasuaji katika hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dk Francis Semwene, alisema majeruhi wawili hali .zao ni mbaya, na wengi wa majeruhi wameumia zaidi maeneo ya kichwani, mikononi na maeneo ya ndani ambapo walikuwa wakiendelea kupata huduma zikiwemo za kushonwa majeraha mbalimbali katika miili yao.

Akizungumza na waandishi wa habari katika eneo la tukio, Mkuu wa wilaya ya Mvomero, Anthony Mtaka aliwaasa madereva kuheshimu sheria za usalama barabarani, na kwamba eneo hilo kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya ajali huku visingizio vikiwa ni utelezi wa barabara.

Mtaka mbali na kutoa pole kwa familia za watu waliopoteza maisha na majeruhi katika ajali hiyo Mbaya, alisema kisingizo cha utelezi hakiwezi kuwa na nafasi kwa wakati huu wa kiangazi, na kwamba uzembe wa madereva ndio umekuwa ukisababisha ajali za mara kwa mara zinazoweza kuepukika.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kijiji cha Wami Sokoine, Marco Ndesse, aliiomba Serikali kuweka matuta katika eneo hilo ambalo ni la makazi, na ambalo lina wananchi wengi wakiwemo watoto, ambao wamekuwa wakivusha mara kwa mara kwenda kuchota maji upande wa pili kwenye lambo.

Alisema magari katika eneo hilo yamekuwa yakipita kwa kasi kubwa, na mara kwa mara kumekuwa kukitokea matukio ya ajali ambazo zinaweza kudhitiwa kwa matuta.

Chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa Noah kujaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake, huku akiwa mwendo kasi  na kabla hajalipita alikutana na lori hilo na hivyo kugongana uso kwa uso na Noah kupinduka.

jumamtanda blog 

0 comments:

Post a Comment