.

.
Wednesday, November 13, 2013

2:14 AM
Na Bertha Ismail –Hanang.

Baada ya kukamilika kwa miundombinu ya  barabara  kwa kiwango cha lami, kutoka Minjingu-Babati hadi Singida Mkoani Manyara hatimaye serikali ya mkoa huo iko mbioni kuanza ujenzi wa kiwanja cha ndege cha kisasa kinachotarajiwa kuanza kujengwa wilayani Babati.
Kwa mujibu wa mkuu wa Mkoa huo, Elaston John Mbwillo, kwa sasa serikali mkoani humo imeomba wataalam kutoka wizarani kuja kukagua maeneo yaliyopendekezwa ya Endakiso na Magugu ili kujua hali ya mazingira ya uelekeo wa upepo.
Mbwillo ametaja baadhi ya malengo ya kujengwa kwa uwanja huo kuwa  ni kupunguza gharama za kuwapokea wageni pamoja na viongozi mbalimbali wakiwemo wa serikali wanaokuja mkoani humo na pia kutoa fursa kwa wawekezaji kuweza kuwekeza.
“Malengo makubwa ya kutaka kujenga uwanja wa ndege hapa mkoani kwetu ni pamoja na kupunguza gharama za kwenda kuwapokea wageni wetu wakiwemo viongozi wa serikali kwani tumekuwa tukilazimika kwenda hadi Arusha kuwapokea viongozi wanaotaka kufika kwetu hali ambayo imekuwa ikitulazimu kujaza magari yetu mafuta ya kutembea umbali wa kilometa zaidi ya 150 kwa gari moja,”Alisema mkuu huyo na kuongeza,
“Na kama unavyojua mapokezi ya kiongozi wa serikali huwezi kufanya mwenyewe lazima uwe na maafisa usalama na baadhi ya wakuu wa idara…si unaona ilivyo ghamara kubwa, matokeo yake tutakuwa tunatumia rasilimali nyingi kwa kitu kimoja”.Alisema Mbwilo.
Alisema kuwa mbali na gharama pia wanakuwa  hawana uhakika na usalama wa wageni wao kwani maafisa usalama wanaowapokea si mkoa wake pia wananchi wanaopishana nao hawafahamiani sambamba na baadhi ya maeneo wanayopitishwa.
Mbwilo aliongeza kuwa mbali hayo pia mkoa wa Manyara ukimiliki uwanja wake wa ndege utasaidia kulinda uchumi wa mkoa ikiwemo biashara kuwepo.
Kwa mujibu wa taarifa ya miundo mbinu ya mtandao wa barabara mkoani humo,kwasasa umefanikiwa kuwa na mtandao wa barabara uliojengwa kwa kiwango cha lami wenye urefu wa km 203.7 kati ya mtandao wenye km 6,010.
Aidha baadhi ya wakazi wilayani Babati Ali Hamza mkazi wa mji mdogo wa Magugu amesema taarifa ya ujenzi huo ilianza kuzungumzwa kwenye majukwaa ya siasa na vikao mbalimbali kwa takribani miaka 10 sasa,lakini endapo ujenzi huo utafanyika basi utasaidia kupanda kwa uchumi wa mkoa huo na wananchi wake.
Hata hivyo licha ya kuwepo kwa mkakati wa kujengwa kwa uwanja huo,kwasasa mkoa huo una vituo vidogo vya ndege 49 (airstrips) katika maeneo ya wilaya zote tano vinavyoruhusu kutua kwa ndege ndogo kwa ajili ya kusaidia kusafirisha watalii.
Fursa nyingine ni kusafirisha wagonjwa waliopata rufaa na flying doctors wanaotumika kuokoa maisha ya majeruhi kabla ya kufikishwa hospitalini.
MWISHO



0 comments:

Post a Comment