.

.
Monday, November 25, 2013

10:38 AM
DAR ES SALAAM. 
SIKU moja baada ya Kamati Kuu ya Chadema kumvua uongozi aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Taifa wa chama hicho, Zitto Kabwe, mama yake mzazi, Shida Salum ametoa ya moyoni akieleza kuwa kilichomkuta mwanaye kimefunika mabaya mengi yaliyopangwa afanyiwe.

“Kwa upande wangu naona kama ni ushindi kwa Zitto kutokana na jinsi ninavyojua hali ilivyo, mambo yalikuwa ni mengi mno na nikwambie tu, Zitto kuvuliwa uongozi kumefunika hayo yaliyokuwa yamekusudiwa kufanywa dhidi yake. Nilikuwa naomba Mungu  kila siku ili afukuzwe Chadema,” alisema mama huyo wakati akizungumza na gazeti hili nyumbani kwake Tabata, Dar es Salaam.
Shida Salum alisema kuwa Mungu amemnusuru mwanaye na kusisitiza, “Watu walikaa na kutengeneza ripoti ya siri kuhusu Zitto na kuiweka kwenye mtandao kisha kuituma kwa wanachama wa Chadema wanaowafahamu. Mpaka wanafikia hatua hiyo maana yake ni kwamba wamejaribu njia zote za kummaliza, lakini wameshindwa.”
Alisema kutokana na hali ilivyo hivi sasa amemnyang’anya mwanaye kwa muda simu zake zote za mkononi, kompyuta mpakato (Laptop) pamoja na iPad ili asiwasiliane na watu, kwa maelezo kuwa wapo wenye nia mbaya wanaomsaka kumpa pole za kinafiki. “Kwa sasa nataka mwanangu atulize akili.”
Shida Salum, mbali na kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, pia ni  mwasisi wa  Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu (Shivyawata) na Mwenyekiti wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa Viungo (Chawata).
Zitto pamoja na Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, Dk Kitila Mkumbo juzi walivuliwa uongozi kutokana na uamuzi wa kikao cha Kamati Kuu kilichokutana kwa siku mbili, kuanzia Novemba 20 mwaka huu katika Ukumbi wa Blue Pearl jijini Dar es Salaam, wakituhumiwa  kukisaliti chama.
Mbali ya kuwavua uongozi Zitto, Dk Mkumbo pamoja na  aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho mkoani Arusha, Samson Mwigamba, pia Kamati Kuu imewapa siku 14 wajieleze kwa nini wasifukuzwe uanachama.
Kwa uamuzi huo Zitto amebaki na wadhifa wa ubunge wake wa Jimbo la Kigoma Kaskazini na Uenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
Katika ufafanuzi wake wa jana, Shida aliwataka wanachama wa Chadema kuwa watulivu kwa maelezo kuwa Zitto hajafukuzwa uanachama, “Siku nyingi walikuwa wanamwinda na hata hilo jambo ambalo Chadema wanasema amefanya, hawana uhakika nalo.”
Juzi wakati akisoma uamuzi wa Kamati Kuu,  mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu alisema wamebaini kuwapo kwa mkakati mkubwa wa watu hao kutimiza malengo hayo ambao umeandikwa katika waraka unaoitwa ‘Mkakati wa Mabadiliko 2013’, ambao umeandaliwa na kikundi kinachojiita ‘Mtandao wa Ushindi’.
Alisema kikundi hicho vinara wake wapo wanne,  Zitto anajulikana kama Mhusika Mkuu (MM), Mkumbo (M1), Mwigamba (M3) na mtu mwingine wa nne ambaye alieleza kuwa hajatambulika na anatumia jina la M2.
 MWANANCHI

0 comments:

Post a Comment