.

.
Thursday, March 6, 2014

12:23 AM
Ridhiwani Kikwete.


CHANZI
Mshindi wa kura za maoni za kugombea ubunge wa Jimbo la Chalinze kwa tiketi ya CCM, Ridhiwani Kikwete amesema siasa anazofanya sasa hazina uhusiano wala ubia na baba yake.

Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kutangazwa kwa matokeo ya kura za maoni za chama hicho katika jimbo hilo kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Msata alisema anafanya siasa kwa maisha yake na si kwa mgongo wa baba yake kwani aliingia katika siasa akiwa na umri wa miaka mitano na hakuwahi kufanya hivyo kwa sababu ya baba yake.

“Siasa ninayofanya haina uhusiano na baba yangu, nafanya siasa kwa maisha yangu na sina ubia na baba yangu katika hili” alisema mtoto huyo wa Rais Jakaya Kikwete.

Akijibu swali la kwa nini amejiingiza katika siasa tofauti na maneno yake aliyowahi kutamka mwaka 2010 kuwa hawezi kushiriki katika kinyang’anyiro cha ubunge katika jimbo hilo, Ridhiwani alisema wakati huo hakuwa tayari.

“Kwenye siasa usiwe muwazi katika kila kitu, ukiwa hivyo unawapa nafasi maadui kukushambulia, mimi hapa Chalinze ni kwetu, kwa wazazi wangu na kule Bagamoyo tunakwenda tu kikazi na ndiyo maana nikaamua kurudi nyumbani kuomba ridhaa. 

Nashukuru kuongoza katika kura za maoni ninaona ni kiasi gani ninaungwa mkono,” alisema.

Katika kura hizo za maoni Ridhiwani alibuka mshindi kwa kura 758, akifuatiwa na Imani Madega aliyepata kura 335, Ramadhan Maneno (206) na Mkwazu Changwa (17).

Kamati Kuu ya CCM (CC), inatarajiwa kukutana Machi 8, mwaka huu kupitisha jina mgombea wake wa ubunge katika jimbo hilo nafasi ambayo iliachwa wazi na Said Bwanamdogo aliyefariki dunia Januari 22, mwaka huu.MWANANCHI

0 comments:

Post a Comment