.

.
Thursday, May 29, 2014

4:03 AM
Dar es Salaam. 
 Suala la kukwama kufungwa kwa ndoa ya Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Vicky Kamata limechukua sura mpya baada ya mzazi mwenza wa mchumba wa mbunge huyo, kukanusha taarifa kwamba alikwenda Dodoma kwa lengo la kuomba msaada kwa viongozi wa Bunge.
Kauli ya mama huyo imezidisha utata katika sakata la kukwama kufungwa kwa ndoa hiyo iliyokuwa ifanyike Jumamosi baada ya kutokea habari kuwa mwanamke mmoja alikwenda bungeni mjini Dodoma kutaka kuonana na Spika kwa lengo la kuomba Bunge limsaidie kupata haki yake kabla ya harusi hiyo kufungwa na hivyo kusababisha harusi kutofanyika.
Kamata, ambaye alijizolea umaarufu kutokana na wimbo wake wa “Wanawake na Maendeleo” na baadaye kuingia bungeni katika uchaguzi wa mwaka 2010, alikuwa afunge ndoa na mtu aitwaye Charles Gardiner Jumamosi iliyopita jijini Dar es Salaam, lakini haikufanyika kutokana na mbunge huyo kuwa mgonjwa kiasi cha kulazwa hospitali maeneo ya Tabata.
Jana, Kinavi Dadi, ambaye ni mzazi mwenza wa Gardiner, alikanusha kufunga safari hadi Dodoma kwa lengo hilo.
“Ni kweli kwamba Charles ni baba watoto wangu, lakini sijawahi kwenda Dodoma na wala sifahamu chochote kuhusu safari hiyo. Nadhani inatosha,” alisema mama huyo na hakutaka mazungumzo zaidi.
Baadaye kidogo mmoja wa ndugu wa Kinavi, ambaye aliomba asitajwe jina lake gazetini, alikiri ndugu yao kufunga ndoa na Gardiner Juni 2004 na kujaliwa kupata watoto wawili, lakini walitofautiana na baadaye ndoa yao kuvunjwa mwaka 2012.
“Ni kweli kwamba dada yetu alifunga ndoa na Charles, lakini pia ni kweli kwamba walipeana takala halali two years ago (miaka miwili iliyopita), kwa hiyo taarifa kwamba eti amezuia ndoa isifungwe, siyo za kweli na wala huko Dodoma hajawahi kwenda,” alisema.
Alisema taarifa kwamba aliyepata kuwa mke wa Gardiner alikwenda Dodoma kuomba msaada wa Bunge zimewaumiza sana kama familia kutokana ukweli kwamba Kinavi ndiye anayefahamika kuwa mke wa kwanza.
“Ndugu yetu analia sana kutokana na kuumizwa na wale wanaomchafua. Sisi katika familia tumelelewa kwa maadili hivyo Kinavi siyo mtu wa kuzuia ndoa ya Gardiner maana walishatengana, mawasiliano yaliyopo ni yale yanayohusu watoto ambao wana haki ya wazazi wote wawili. Hatujui waliozitangaza hizo habari walikuwa na malengo gani,” alisisitiza.
Bungeni Dodoma
Wakati hayo yakiendelea, habari kutoka bungeni Dodoma zinasema mwanamke aliyedaiwa kuwa mke wa Gardiner ni ‘feki’ na alikuwa wa kutengenezwa na baadhi ya wabunge kwa lengo la kumtibulia Kamata.
Mpango huo unadaiwa kuwahusisha wabunge wanawake wanne; watatu kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) na mmoja kutoka Chadema ambao awali waliapa kwamba ndoa ya mbunge mwenzao isingefungwa.

0 comments:

Post a Comment