.

.
Tuesday, March 12, 2013

2:49 PM
Erasto Nyoni kushoto akimtoka beki wa Cameroon, Assou Ekotto katika mchezo wa kirafiki Februari 6, mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Je, ataendelea kuitwa Stars japo hachezei timu yoyote?

Na Prince Akbar
KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Kim Poulsen kesho anatarajia kutaja kikosi chake kitakachoivaa Morocco, kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil.
Poulsen, atataja kikosi hicho kinachosubiriwa kwa hamu na wadau katika Mkutano na Waandishi wa Habari utakaofanyika asubuhi ya kesho kwenye ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), zilizopo ndani ya Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam. 
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, bia inayozalishwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), itacheza na Morocco kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Machi 24 mwaka huu.
Katika kikosi hicho, Watanzania wanasubiri kuona kama Poulsen ataendelea kuwaita mabeki Aggrey Morris na Erasto Nyoni ambao hawajacheza Ligi Kuu mwaka huu kutokana na kusimamishwa na klabu yao Azam FC.
Wachezaji hao walisimamishwa kwa pamoja na kipa Deo Munishi ‘Dida’ na beki mwingine, Said Mourad kwa tuhuma za kuihujumu timu yao katika mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu mwaka jana.
Kim aliendelea kuwaita wachezaji hao katika mechi zilizopita ingawa wadau wamekuwa wakilaani kitendo hicho. 
Tanzania bado ina nafasi ya kukata tiketi ya Brazil mwakani, kwani hadi sasa inashika nafasi ya pili kwenye kundi lake, kwa pointi zake tatu nyuma ya Ivory Coast inayoongoza kwa pointi zake nne.
Hadi sasa, Stars imecheza mechi mbili, imeshinda moja nyumbani dhidi ya Gambia 2-1 na kufungwa moja na Ivory Coast ugenini 2-0.
Morocco wanashika nafasi ya tatu kwa pointi zao mbili, wakati Gambia yenye pointi moja inashika mkia na timu zote katika kundi hilo zimecheza mechi mbili mbili kila moja.    

KUNDI C:
                                P W D L GF GA GD Pts
1 Ivory Coast 2 1 1 0 4 2 2 4
2 Tanzania               2 1 0 1 2 3 -1 3
3 Morocco                2 0 2 0 3 3 0 2
4 Gambia 2 0 1 1 2 3 -1 1

REKODI YA STARS TANGU MWAKA JANA:
Februari 23, 2012
Tanzania 0 – 0 DRC (Kirafiki)
Februari 29, 2012
Tanzania 1 – 1 Msumbiji (Kufuzu Mataifa ya Afrika)
Mei 26, 2012
Tanzania 0 – 0 Malawi
Juni 2, 2012
Ivory Coast 2 – 0 Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 10, 2012
Tanzania 2 – 1 Gambia (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 17, 2012
Msumbiji 1 – 1 Tanzania (Tanzania ilitolewa kwa penalti kufuzu Mataifa ya Afrika)
Agosti 15, 2012
Botswana 3 – 3 Tanzania (Kirafiki)
Novemba 14, 2012
Tanzania 1-0 Kenya (Kirafiki)
Desemba 22, 2012
Tanzania 1-0 Zambia (Kirafiki)
Januari 11, 2013
Tanzania 1-2 Ethiopia (Kirafiki)
Februari 6, 2013
Tanzania 1-0 Cameroon (Kirafiki)

MECHI ZIJAZO:
Machi 22, 2013
Tanzania Vs Morocco (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 7, 2013
Morocco Vs Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 14, 2013
Tanzania Vs Ivory Coast (Kufuzu Kombe la Dunia)
Septemba 6, 2013
Gambia Vs Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
chanzo: bin zubery

0 comments:

Post a Comment