.

.
Monday, March 11, 2013

8:07 AM
Pichani juu. Baadhi ya askari wakifyeka mimea ya madawa
ya kulevya aina bangi iliyolimwa kwenye moja ya bonde lililopo katika kijiji cha Likamba wilayani Arumeru

Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
Siku chache tu baada ya Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya Usalama Mkoani hapa kuendesha operesheni ya nguvu ya uteketezaji wa madawa ya kulevya aina ya bangi iliyopo kwenye baadhi ya mashamba yaliyopo wilayani Arumeru, sasa hali hiyo imechukua sura mpya baada ya wananchi wa maeneo hayo kuungana na askari wa jeshi hilo kuteketeza madawa hayo.
Hali hiyo ambayo haijawahi kutokea, imekuja baada ya viongozi wa jeshi hilo kukaa pamoja na wananchi hao na kutumia dhana ya ulinzi shirikishi kwa kuwaelimisha wananchi hao juu ya madhara ya madawa hayo ya kulevya hali ambayo imesaidia kuwahamasisha kuamua kuingia mashambani kufyeka bangi hiyo.
Baadhi ya wakazi wa vijiji vya Likamba na Imbibya wilayani humo,  walisema kwamba mbali na kauli ya jeshi hilo kwamba operesheni  hiyo itakuwa endelevu pia wamegundua madhara ya madawa hayo.
“Japokuwa tunafanya biashara ya madawa hayo kwa kuuza kwa kila gunia kwa Tsh 130,000 hadi 150,000 lakini tunaona biashara hii haina uhuru badala yake inatufanya tuishi kwa hofu kila wakati na pia tumegundua yana madhara makubwa kwa afya ya binadamu”. Alisema mkazi mmoja wa kijiji cha Imbibya ambaye hakutaka kutaja Jina lake.
Baada ya kufanikiwa kukamata kwa madawa hayo jumla ya magunia 143 ambayo yalikuwa yanasafirishwa kwenda maeneo mbalimbali ya ndani na nje ya nchi yetu, jeshi hilo mkoani hapa limeamua kufanya operesheni endelevu ya kuingia mashambani ambapo rasmi ilianza tarehe 01.03.2013.
Mwandishi wa habari hii alihakikishiwa na Kamanda wa polisi wa Mkoa huu Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Liberatus Sabas kuwa jeshi lake limewasha “moto” ambao hautazimika juu ya Operesheni hiyo na litaendelea kufanya hivyo mpaka wahakikishe mashamba yote ya madawa hayo yanateketezwa na kuwataka wakazi wa maeneo mengine waanze kuteketeza madawa hayo kama wanavyofanya wenzao wa vijiji vya Likamba na Imbibya.
Alisema katika operesheni ya mara ya pili iliyofanyika tarehe 04.03 mwaka huu waligundua kuwepo kwa mimea ya madawa hayo katika bonde linalotenganisha vijiji hivyo ambayo waliifyeka na kisha kuichoma moto na kufanya jumla ya hekari 120 kuharibiwa kwa siku hiyo.
Tangu operesheni hiyo ya kuteketeza madawa hayo ya kulevya aina ya bangi ianze kwa siku mbili tofauti imeonyesha mafanikio makubwa ambapo mpaka sasa jumla ya mashamba yanayokadiriwa kuwa na hekari 270 toka vijiji vya Likamba na Imbibya vilivyopo wilayani Arumeru zimeharibiwa kwa kufyeka na kuteketeza kwa moto.

0 comments:

Post a Comment