.

.
Sunday, March 31, 2013

2:23 PM


Rais Jakaya Kikwete akifuatilia zoezi la uokoaji kwenye jengo la ghorofa 16 lililoanguka katika Mtaa wa Indira Gandhi jana. Kulia ni Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova na Mkurugenzi wa Kitengo cha Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Meja Jenerali, Sylvester Rioba.


Zoezi la kutafuta miili iliyokwama katika vifusi inaendelea, zaidi ya maiti 22 zapatikana.
Dar es Salaam. Idadi ya watu waliokufa kutokana na kufukiwa na kifusi cha jengo la ghorofa 16 lililoporomoka juzi asubuhi jijini Dar es Salaam, imefikia 22.
Habari zilizopatikana kutoka eneo la uokoaji na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova zinaeleza kuwa miili iliyopatikana imepelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Jengo hilo lililokuwa likijengwa mkabala na Msikiti wa Shia Ithnasheri ulioko Barabara ya Indira Gandhi na Kampuni ya Lucky Construction Limited liliporomoka saa 2.30 asubuhi wakati mafundi na vibarua wakiendelea na ujenzi huku chini watoto wakicheza mpira na mama lishe wakiendelea na biashara zao kama kawaida.
Rais Kikwete
Rais Jakaya Kikwete ambaye jana pia alifika katika eneo la tukio, kama ilivyokuwa juzi, alipata taarifa fupi ya maendeleo ya uokoaji kutoka kwa Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadik na Kamanda Kova.

Baada ya kupewa taarifa hiyo, Rais Kikwete alimwagiza Kamanda Kova kuhakikisha wahusika wanakamatwa akiwamo Mkadiriaji Majengo (Quantity surveyor), mchora ramani za majengo (Architecturer), Mhandisi Mshauri (Consultant) na Mhandisi wa Jiji la Dar es Salaam. Juzi baada ya kutembelea eneo la tukio, Rais Kikwete aliagiza wahusika wote wa ujenzi huo wachukuliwe hatua kali.
Habari zilizopatikana jana zilidai kuwa Diwani wa Kata ya Goba, Wilaya Kinondoni, Ibrahim Kisoka ambaye ndiye mmiliki wa kampuni ya ujenzi, na Mhandisi Mshauri kwa pamoja wamejisalimisha Kituo Kikuu cha Polisi na hadi saa 8:00 jana mchana walikuwa wakihojiwa.
Awali Kamanda Kova aliwaambia waandishi wa habari kuwa amemtaka mmiliki wa Kampuni ya Lucky Construction Limited ambaye ni Diwani wa Kata ya Goba, Kisoka na wahusika wengine kujisamilisha kituo cha polisi, kabla hawajaamua kutumia nguvu kumtafuta.
Pinda atembelea eneo la tukio
Waziri Mkuu Mizengo Pinda alifika eneo hilo saa 3:41 asubuhi, kujionea hali ilivyo, lakini hakutoa tamko lolote. “Sina la kusema,” alisema Waziri Mkuu alipoulizwa na waandishi wa habari kutoa kauli ya serikali kuhusiana na tukio hilo.

Hata hivyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi aliyefuatana na Pinda, alisikika akimwagiza Kamanda Kova kuhakikisha mchora ramani wa jengo hilo naye anatiwa nguvuni kwa kuwa jengo hilo lilikuwa la ghorofa 10, lakini likajengwa hadi 16. Mtu mwingine ambaye anatafutwa na jeshi la polisi kukamatwa ni Mhandisi Mshauri.
Lukuvi alimwagiza Kova kuwa watu waliokuwa karibu na jengo jingine la ghorofa 15 lililojengwa na mkandarasi huyo, kuhama mara moja na ubomoaji ufanyike bila kuleta madhara.
Mwenyekiti wa CUF
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba alitumia fursa hiyo kuitaka Serikali kuwabana makandarasi wasio na sifa kwani wanahatarisha maisha ya watu.
“Huu ni uzembe, wahandisi wa jiji walikuwa wapi? Wasimamizi na washauri walikuwa wapi hadi jengo linafikia ghorofa 16?” Alihoji Profesa Lipumba.

Profesa Lipumba aliitaka Bodi ya Makandarasi (CRB) kufuta leseni ya kampuni hiyo, kwani imeonyesha kuwa haiwezi kusimamia ujenzi na hivyo kusababisha vifo.
chanzo:mwananchi

0 comments:

Post a Comment