.

.
Friday, September 27, 2013

4:45 AM
                                                                                         na Grace Macha, Arusha

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, amesema serikali inashughulikia maombi ya mwekezaji kwenye kinu cha kusaga na kukoboa nafaka cha Arusha (NMC), Kampuni ya Monaban ya kuomba kuongezewa mkataba au kuuziwa kiwanda hicho.
Aidha, alimpa pole kwa madai aliyomweleza ya kupata usumbufu kutoka kwa watendaji wa serikali ambao walifikia kuzima mashine wakati akiwa anaendelea na usagaji wa nafaka jambo lililosababisha bidhaa hizo kuharibika.
Pinda alitoa kauli hiyo juzi baada ya kutembelea kiwanda hicho na kujionea shughuli za ukoboaji na usagaji wa mahindi na ngano zilivyokuwa zikiendelea pamoja na kuona ghala la uhifadhi wa bidhaa hizo.
“Nimeona unasononeka na kuumizwa sana na uamuzi wa vinu vingine kuuzwa na hiki hakikuuzwa, uamuzi ulifikiwa baada ya kuunda bodi ya nafaka na mazao tukaona hiki na kile cha Iringa tusiviuze viendelee kusimamiwa na bodi hii.
“Nimeona umewekeza, umefunga mashine mpya, lakini ombi lake Bwana Molel, apewe kipindi kirefu zaidi au auziwe hiki kiwanda, tumeshaongea na watu wa kilimo ili watazame na sisi tutaangalia,” alisema.
Pinda aliongeza kuwa huo ndio mchango wa serikali kwenye uwekezaji, japo wakati mwingine wakiwekeza kwenye mali za umma wale wanaowekwa wasimamie wanaziua zaidi.
Alipongeza jitihada za Kampuni ya Monaban katika kukifufua kiwanda hicho sanjari na kushiriki ipasavyo katika kununua mahindi ya wakulima mpaka ngazi wa chini vijijini, ambapo ameuza mahindi tani 7,600 kwa wakala wa ghala la chakula la taifa Kanda ya Kaskazini kwa msimu huu wa kilimo.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Monaban, Philip Mollel, alisema kuwa mwaka 2007 aliingia mkataba wa miaka 15 wa kufufua kinu cha ngano kilichokuwa kimekufa kwa zaidi ya miaka 10 na kukarabati kinu cha mahindi ambapo ametumia zaidi ya sh bilioni 6.2 kufanya kazi hiyo.
“Mkataba nilioingia ni wa kufufua, kukarabati, kuendesha na kuzalisha unga wa ngano na mahindi hapa NMC Arusha kwa miaka 15, ambapo baada ya kipindi hicho kampuni yetu inaweza kuingia mkataba mwingine,” alisema.
Hata hivyo alisema kuwa kampuni yake inashindwa kufanya maboresho zaidi, ikiwamo kufunga mitambo mikubwa zaidi, kuweka lami eneo la ndani ya kiwanda na kujenga uzio imara wa matofali ya saruji kuzunguka kiwanda hicho kutokana na kukosa ushirikiano kutoka serikalini.
Hali hiyo alidai inasababishwa na urasimu anaofanyiwa na Shirika Hodhi la Mitaji (CHC) ambalo hutumia waraka namba 40 wa serikali kumzuia asinunue kiwanda hicho wakati waliuza viwanda vingine kwa wafanyabiashara wenye asili ya Asia baada ya waraka huo kuwa umetolewa.
“Hivi majuzi Agosti 31, mwaka huu CHC bila kunipa taarifa huku wakijua nimewekeza walikuja kiwandani kwa lengo la kukabidhi kiwanda kwa bodi ya nafaka na mazao mchanganyiko.
“Walifanya hujuma ya kuzima mashine bila taarifa wala ridhaa yangu. Mpaka sasa sijaelewa lengo lilikuwa ni nini. Uzimaji huo uliisababishia Monaban hasara kubwa sana hasa ukizingatia kuwa tani 120 za ngano na 60 za mahindi zote kwa pamoja zilikuwa tayari kwenye mfumo na mchakato wa uzalishaji hivyo nafaka hizo ziliharibika,” alisema

0 comments:

Post a Comment