.

.
Friday, September 6, 2013

1:01 PM

Na Bertha Ismail.

 

 
Ikiwa ni siku chache tangu taarifa zizagae juu ya mtalii raia wa Marekani kuuawa na kundi la Tembo katika hifadhi ya Tarangire, TANAPA wamekanusha vikali taarifa hizo za mtalii huyo kufia katika hifadhi zao.

 

Akikanusha taarifa hizo, Meneja uhusiano wa Tanapa, Paschal Shelutete, alisema kuwa eneo alilokuwa mgeni huyo ni nje ya hifadhi yao ambapo waliwaona kundi hilo la tembo na kutaka kuwapiga picha ndipo Tembo hao kuwageukia ambapo  watalii hao walianza kukimbia ndipo marehem alipoanguka kwenye tope ambapo Tembo hao walipita juu yake.

 

“Tukio la mgeni husika lilitokea nje ya hifadhi ya Tarangire katika kijiji cha Kakoi kambi ya Tarangire River Camp, wakiwa wanafanya utalii wa kutembea kwa miguu na siyo amefia katika hifadhi zetu kama baadhi ya watu wanavyodai.”

 

“Aidha Baada ya kuvamiwa na kuumizwa, mgeni huyu alifikishwa katika zahanati ya Tarangire na watumishi wa kambi aliyofikia ambayo iko nje ya hifadhi kwa ajili ya matibabu ya huduma ya kwanza ambapo alifariki,” alisema Shelutete.

Aidha taarifa ya TANAPA imekuja baada ya hivi karibuni mtalii mmoja raia wa Marekani, Thomas Macfee (58), kuuawa na kundi la tembo wakati akiwa kwenye kambi ya Kakoi Tarangire eneo linalodaiwa kuwa ni mapito ya asili ya wanyama hao lililoko ndani ya hifadhi ya Tarangire.

 

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Manyara, Musa Marambo, alipokuwa akitoa taarifa yake kwa waandishi wa habari hivi karibuni, alisema kuwa tukio hilo limetokea Agost 30 majira ya  saa 2:30 asubuhi baada ya mtalii huyo akiwa na wenzake watano ambao majina yao hayakupatikana kwa haraka  kujaribu kupiga picha kundi kubwa la tembo lililokuwa likipita karibu na eneo la hifadhi walilokuwa.

 

Alisema kuwa wakiwa kwenye harakati za kupiga picha, ghafla tembo hao walibadili uelekeo na kuanza kuwafuata ndipo wakaanza kukimbia ambapo kwa bahati mbaya marehem (Macfee) alinasa kwenye dimbwi la matope.

 

“Baada ya kunasa kwenye matope alishindwa kutoka ndipo tembo wale wakaanza kumpitia juu na baada ya tembo hao kuvuka  wenzake walimfuata na  kumchukua na kumuwahisha kwenye zahanati ya hifadhi ya taifa ya Tarangire ndipo akafariki,” alisema Marambo.

 

Alisema kuwa baada ya kufariki alipelekwa kuhifadhiwa kwenye hospitali ya Selian jijini Arusha ambapo ubalozi wa Marekani ulimchukua kwa ajili ya taratibu za mazishi nchini marekani.

0 comments:

Post a Comment