.

.
Tuesday, December 3, 2013

12:33 PM

AMIRI Jeshi Mkuu, Rais Dk, Jakaya Kikwete, ametoa wiki mbili kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya ujambazi, wakiwamo wanaomiliki silaha kinyume cha sheria na wahamiaji haramu kujisalimisha na silaha zao.
Alisema kwa kuwa amechoshwa na matukio yao, baada ya hapo kwa wale watakaoshindwa kutekeleza amri hiyo, msako mkali utakaofanyika ukiyahusisha majeshi yote utawan

asa.
Dk. Kikwete alitoa tamko hilo jana wakati akihutubia wananchi wa Wilaya ya Biharamulo, baada ya kuweka jiwe la msingi katika barabara ya Kagoma- Lusahunga inayojengwa na Serikali kwa asilimia 100.

“Nasema mchana kweupe, macho makavu nimechoshwa na kukasirishwa na vitendo vinavyofanywa na baadhi ya watu vya kuteka magari katikati ya pori la Kasindaga, sasa nawataka wale wote walio miongoni mwa makundi niliyotaja wachukue maamuzi haraka...Watanzania hatuwezi kukubali  wasafiri bila amani,” alisema Kikwete.

“Sina mzaha kwa hili atakayekaidi kufuata ushauri huo, baada ya wiki mbili utaanzishwa msako mkali, tutawasaka msituni, majumbani hadi wanapoficha silaha zao na risasi. Msako huo utahusisha majeshi yote likiwemo jeshi la polisi, jeshi la wananchi na usalama wa Taifa na vyombo vingine vya ulinzi na usalama tutawasaka kotekote, hakuna mahali pa kukimbilia...,” alisema.

Alisema hali ya ujambazi imekithiri katika mikoa ya Geita, Kagera na Kigoma. Alisema lengo la msako huo ni kukomesha vitendo hivyo ambayo vimekuwa kero kubwa kwa wananchi wanaotumia barabara hiyo.
“Ole wao watakaowafyatulia risasi askari wangu, wakamatwe mateka na jeshi kwa lugha ya kijeshi mtanielewa," alisisitiza.

Aidha, aliwatahadharisha Watanzania wanowahifadhi na kushi
rikiana na majambazi hao waache mara moja na kutafuta kazi nyingine ya kufanya kabla hawajakumbwa na dhahma hiyo.

Wakati huo huo, Rais Kikwete aliweka jiwe la msingi katika barabara ya Kagoma Lusahunga yenye urefu wa kilomita 154 iliyojengwa kwa ufadhili wa Serikali kwa silimia 100.

Alisema kuwa lengo la kujenga barabara kwa kiwango cha lami ni kuhakikisha Tanzania inafunguliwa kiuchumi.

Aliwashauri wakandarasi wa Tanzania kuiga mfano wa kampuni iliyojenga barabara ya  mfano kutoka China (Chico) kwa kazi nzuri  yenye viwango.

Aliiomba kampuni hiyo kuwa wavumilivu wakati Serikali ikiendelea kushughulikia madai yao ya Sh. bilioni 40 zilizobaki Serikali.

Rais alitoa kauli hiyo baada ya Waziri wa Ujenzi, John Magufuli kumweleza kuwa hajawahi kumsifia mkandarasi yeyote lakini hao wamefanya kazi nzuri, na kuonyesha moyo huku wakitarajia kukamilisha mradi huo kwa wakati kwa muda wa miezi 36 kama ilivyopangwa.

Kwa upandewa  Mtendaji mkuu wa wakala wa barabara Tanzania (Tanroad), Alon Mugale, alisema mradi huo ulianza mwaka 1995 ikiwa ni upembuzi yakinifu na kwa sasa imefikia asilimia 96 ya ujenzi.

Alisema  kilomita 153.5 zimekamilika bado meta 500 zitakazokamilika mwishoni mwa mwezi Agosti, mwaka huu na kugharimu Sh. bilioni 191.4.

CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment