.

.
Tuesday, December 3, 2013

12:29 PM
Matukio ya ubakaji kushamiri Manyara.

Na Bertha Ismail- Manyara

Kuongezeka kwa matukio ya ubakaji kila mwaka Mkoani Manyara, jeshi la polisi mkoani humo limekiri kuwa changamoto kwao.


Aidha hali hiyo imedhihirika wakati jeshi la polisi mkoani Manyara likiwa katika wiki ya  kuadhimisha miaka 16 za kupinga ukatili wa kijinsia ambapo ripoti imeonyesha kuwa ubakaji umeongezeka kutoka 102 kwa mwaka jana hadi makosa 132 kwa mwaka huu kuanzia januari hadi septemba.


Akisoma ripori hiyo kwa waandishi wa habari hivi karibuni ofisi ni kwake, kamanda wa polisi mkoa wa Manyara Akili Mpwapwa alisema kuwa katika maadhimisho hayo ya miaka 16 ya kupinga ukatili wa kijinsia, wamefanikiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa matukio ya kiuhalifu lakini makosa ya ubakaji yamekuwa kama changamoto kwa jeshi hilo.


Alisema kuwa kwa makosa yaliyoripotiwa kuanzia januari hadi septemba mwaka huu makosa ya ubakaji yameongezeka hadi kufikia 132 ikilinganishwa na mwaka jana kuanzia januari hadi septemba ambapo yaliripotiwa matukio 102 ya ubakaji.


Alisema kuwa matukio hayo ya ubakaji yamekuwa changamoto kuwba kwa jeshi hilo katika kupambana nalo kwani yamekuwa yakiongezeka mwezi hadi mwezi ambapo matukio hayo kuanzia januari hadi march mwaka jana yaliripotiwa makosa 29 ya ubakaji.


“Matukio haya yamekuwa changamoto kubwa kwa jeshi la polisi kwani pia mbali na kuongezeka kwa mwaka pia kwa misimu ya ripoti zetu za matukio haya ya unyanyasaji wa kijinsia ubakaji umekuwa ukiongezeka siku baada ya siku badala ya kupungua” Alisema Mpwapwa.


“Ukiangalia hapa mwaka jana kuanzia januari hadi march yaliripotiwa makosa 29, ila idadi hiyo imekuwa ikiongezeka kwani ripoti ya April hadi jun yaliongezeka hadi kufikia 38 na julai hadi septemba yaliripotiwa makosa 35” Aliongeza.


Mpwapwa alisema kuwa idadi ya makosa hayo kwa mwaka huu yameongezeka tena ambapo katika ripoti ya polisi inaonyesha kuwa, kuanzia  januari hadi march makosa 42 yaliripotiwa Na Idadi hiyo kuongezeka tena mwezi April hadi june na kufikia 46 huku mwezi julai hadi Agost yakiwa ni makosa 44.


Alisema kuwa makosa hayo ya ubakaji yanafuatiwa na makosa mbalimbali ya ulawiti ambapo kwa mwaka huu pia makosa hayo yameongezeka kutoka 9 kwa mwaka jana kuanzia januari hadi septemba ambapo kwa  mwaka huu makosa hayo yamefikia hadi 20 kuanzia januari hadi septemba mwaka huu.


Akitaja makosa ya utupaji watoto wachanga, Mpwapwa alisema kuwa matukio hayo yamekuwa sawa kwani kwa mwaka jana juanzia januari hadi septemba yaliripotiwa makosa 3 idadi ambayo ni sawa na ya mwaka huu.


Mpwapwa alisema kuwa unyanyasaji huu wa kijinsia, jamii imekuwa na ukatili wa aina mbalimbali ambao sehemu kubwa ya waathirika ni wanawake na watoto,

“Unyanyasaji huu unakuwepo sana kwa upande wa akina mama na watoto hasa katika makosa ya kujamiiana, mashambulio ya mwili, ukatili wa kishirikina dhidi ya wenye ulemavu hasa wa ngozi( Albino)”.Alisema Mpwapwa.


“Na haya yanawatokea wanawake na watoto kutokana na uwezo wao hafifu wa kujitetea ambapo wakifanyiwa unyanyasaji huo ni ngumu kujikwamua kwani pia wamekuwa wakizulumiwa mali na pia kubaguliwa sehem za kazi na wao kunyamazia kimya” aliongeza Mpwapwa.


Mpwapwa alisema, jeshi la polisi kupitia dawati la jinsia na watoto baada ya kuona matukio ya kihalifu yanayohusu wanawake na watoto  ni makubwa, serikali kupitia jeshi hilo wanapinga matukio hayo na kudumisha usawa wa kijinsia lengo ni kusaidia watu wote kushiriki katika harakati za kimaendeleo wakiwa huru bila hisia za kubaguliwa wala kuharaulika.


Mpwapwa alisema kuwa mbali na wanawake kuwa miongoni mwa waathirika wa unyanyasaji wa kijinsia ambao wanapaswa kuwa mstari wa mbele kupinga ukatili lakini pia wao ndio wahusika wakubwa wa ukatili kwa watoto kwa kuwaadhibu kikatili.


“pamoja na wanawake kuwa miongoni mwa waathirika wa tatizo hili ambapo ingepaswa wao kuwa mstari wa mbele kuunga mkono juhudi za utokomezaji wa ukatili lakini inasikitisha kuwa wao ndio watuhumiwa wakubwa wa ukatili kwa watoto” Alisema Mpwapwa.


“Watuhumiwa hao wanawake hufikishwa polisi kwa makosa ya kuwaadhibu watoto kwa kipigo cha kinyama, pia kwa kuwachoma moto hali inayosababisha majeraha makubwa kwa mtoto na kuwaathiri kisaikolojia”.


Alisema mbali na adhabu hizo, pia huwa mstari wa mbele kuwafanyia ukatili wa ukeketaji ambapo baada ya dawati la jinsia kugundua na kukemea wanawake hao sasa huwakeketa watoto wao wakiwa wachanga mara tu baada ya kujifungua.


“Mbali na adhabu upo ukatili mwingine wa ukeketaji ambapo baada ya dawati la unyanyasaji na ukatili wa jinsia kukemea, wanawake hao wamegundua njia nyingine ya kuwakeketa watoto wachanga mara tu baada ya kujifungua hali ambayo ni hatari zaidi kwa watoto hao” Alisema Mpwapwa.


Pamoja na kuwepo kwa kauli mbiu ya maadhimisho haya yaliyopendekezwa kitaifa ambayo ni “ Funguka tumia mamlaka yako kuzuia ukatili wa kijinsia, boresha afya ya jamii” lakini jeshi la polisi kupitia dawati la jinsia na watoto mkoani Manyara wanatumia kauli mbiu hiyo pamoja na yao isemayo “ Funguka tumia dawati la kijinsia la polisi kuzuia ukatili wa kijinsia”


Aidha maadhimisho haya ya miaka 16 ya kupinga ukatili wa kijinsia yaliyozinduliwa novemba 25 yatadumu kwa wiki nzima hadi desemba 10 ambapo kwa mkoa wa Manyara jeshi la polisi kupitia dawati la jinsia limetoa msaada wa mashuka 25, sabuni ya unga mfuko mmoja wa kilo 50 na sabuni ya mche box mbili(2) kwenye wodi ya wazazi katika hospitali ya Mrara iliyoko mkoani humo.


Jeshi hilo pia kwa kutambua umuhimu wa wazee wanaofanyiwa ukatili kwa imani za kishirikina pia wamewapa elimu ya kuweza kutoa taarifa juu ya ukatili ambapo katika kituo cha kulelea wazee hao kilichoko Magugu mkoani humo wamepatiwa msaada wa chakula mchele kilo 80, mafuta ya kula lita 10 na sabuni za kufulia za mche na unga.


Mwisho………………


0 comments:

Post a Comment