.

.
Tuesday, April 16, 2013

2:56 AM
1KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdalrahman Kinana na Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC), Nape Nauye, wamezomewa na kulazimika kumaliza mapema mkutano wao katika mji wa Ruaha wilayani Kilosa baada ya kushindwa kujibu maswali ya wananchi.

Kuzomewa kwa Kinana na kundi la viongozi wenzake alilofuatana nalo kulitokana na maswali matatu ya msingi yaliyoulizwa na wananchi, likiwamo aliloulizwa moja kwa moja yeye kuwa anajisafisha vipi kwa Watanzania wakati kampuni yake inatuhumiwa na kuhusishwa na utoroshwaji wa pembe za ndovu kwenda nje ya nchi.

“Mkuu, wananchi hatujaelewa nini unataka kutudanganya wakati wewe kupitia kampuni yako ya usafirishaji unatuhumiwa kutorosha pembe za ndovu nje ya nchi. Hapa kuna tatizo sugu la maji safi na salama kwa miaka mingi na serikali ya chama chako imekuwa inakuja na kutoa ahadi zisizotekelezeka.

“Sasa umekuja na staili gani mpya kutudanganya? Mji huu ni mkubwa, ajabu hauna hata zahanati, unasemaje?” alihoji Francis Leonard, huku akishangiliwa.

Kinana alionesha kuchanganywa na maswali hayo na kujikuta akijibu pasipo wananchi kuridhika, jambo lililoamsha yowe na minong’ono ya chini kwa chini wakisema: “Hawana jipya hawa.”
“Kwanza, nikupongeze kijana. 

Nadhani umetumwa, lakini kwa kifupi ni kwamba kama kuna mtu mwenye ushahidi na hayo aende mahakamani,” alifafanua Kinana kabla hajashauriwa kutelemka na kuachana na hoja hizo.

Kutelemka kwa Kinana kukatoa nafasi kwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Amel Nahadi na Diwani wa Kata ya Ruaha, Rahel Nyangasi, kujibu swali lililohusu hatima ya usugu wa tatizo la maji na zahanati katika mji huo.

Amel alisema tatizo la maji lilitokana na wananchi kuiba pampu ya maji kwenye chanzo, jibu lililopingwa kwa kelele nyingi na wananchi hao wakilazimisha naye kushuka jukwaani.

“Mkubwa, kwa kuwa mpo hapa na mna vyombo vya usafiri twendeni hapo kwenye chanzo, huyu mwenyekiti akawaoneshe pampu iliyofungwa na kuibiwa kwa siku moja. 

“Tuachane na uongo wakati watu tunaumia…sisi tunataka maji, leo tuibe pampu kivipi? Kwani eneo hilo halina mlinzi?” ilisikika sauti ya mtu mmoja na wengine kushangilia.

Baada ya Amel kumaliza, zomeazomea hizo zikahamia kwa Diwani Rahel, ambaye aliimbiwa wimbo wa ‘fisadi…fisadi…fisadi’, hivyo akalazimika kujibu kwa kifupi kuwa zahanati inaanza kazi Aprili 15 mwaka huu, kisha akashuka haraka.

Akionesha kukasirishwa na hali hiyo, Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Morogoro, Innocent Kalogelis, alihitimisha mkutano huo akitoa agizo kwa viongozi wa serikali wa mkoa na wilaya wakiwamo Kamanda wa Polisi wa mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa kuhakikisha mji huo unatawalika, vinginevyo waondoke.

Kauli ya Kalogelis iliwafanya wakazi wa mji huo kumtamkia kuwa hawatishwi na utawala wa kiimla wa chama hicho, huku wakimtaka akajitafakari juu ya matamshi yake.

Katika hali ya kushangaza, baada ya Kinana na viongozi wenzake kuondoka wakielekea Ifakara, wananchi hawakutaka kutawanyika kwenda makwao, bali waliendelea kumsubiri Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) mkoani humo, Susan Kiwanga.

Hatua hiyo ilikuwa ni baada ya kusikia kuwa atapita katika ofisi za chama hicho katani hapo kwa shughuli za kichama akielekea nyumbani kwa wazazi wake Ifakara.

Akiwa amepigwa butwaa kukuta watu wengi wakimsubiri, Kiwanga aliingia ofisini kwa muda mfupi na viongozi wa chama wa Kata ya Ruaha na alipotoka nje wananchi hao walimtaka apande jukwaani awahutubie, wakitaka kujua yaliyojili bungeni.

“Ndugu zangu kwanza niwashukuru kwa heshima hii, ila mkusanyiko huu hatuna kibali,” alisema lakini wananchi walipaza sauti wakimtaka apande jukwaani huku wakimhakikishia ulinzi.

“Tunataka kusikia maneno ya hekima kutoka kwako, tunakuhakikishia kuwa kama wanataka kushuhudia vurugu leo walete polisi wao…kwanza tumechoshwa na utawala wao wa kiimla. Sema mama kuhusu hali ya bungeni,” walimshwawishi.

Kiwanga alikubali ombi hilo, ambapo alisema kwa sasa hali si shwari bungeni na kwamba utawala wa nguvu ndio umedhihirika baada ya Spika kwa makusudi kuwabana wapinzani. 
http://www.freemedia.co.tz

0 comments:

Post a Comment