.

.
Wednesday, April 10, 2013

6:10 AM
http://www.freemedia.co.tzMwigulu Nchemba 
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mwigulu Nchemba.Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare.
SIKU moja baada ya Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mwigulu Nchemba, kukiri kuhusika na video inayomuonesha Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare, maswali mengi yameibuka juu ya kada huo.

Baadhi ya wananchi wamelidokeza Tanzania Daima Jumatano kuwa kwa kukiri huko, Mwigulu alitakiwa kukamatwa na Jeshi la Polisi na kufunguliwa mashtaka kutokana na nyendo zake kuonesha kwamba anahusika na mchezo huo.

Mwigulu alikiri kuwa ndiye aliyeipeleka video ya Lwakatare polisi na kwamba alifanya hivyo baada ya kuripoti kuandikiwa ujumbe wa simu wa kutishiwa maisha na baadhi ya viongozi wa CHADEMA.

Hata hivyo wananchi hao wameibua maswali magumu wakihoji alikoipata video hiyo inayoashiria vitendo vya uchochezi na kwamba iweje msamaria mwema aipeleke kwake badala ya vyombo vya dola.

“Kwanza, Mwigulu ametusaidia kutambua mchezo mzima, kwani tutapaswa kuelezwa yeye ni nani hadi msamaria mwema atoke CHADEMA, ampelekee video inayopanga mauaji badala ya kuipeleka polisi?” alihoji mwanasheria mmoja aliyeomba kuhifadhiwa jina lake.

Mkanganyiko zaidi ulizidi kutawala baada ya Mwigulu kuandika ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa Jamii Forum jana, akidai hausiki kurekodi mkanda wa video ya Lwakatare.

Katika ujumbe wake huo, Mwigulu aliandika: “Ndg wana JF sijashiriki kurekodi mkanda wa video unaomwonesha kiongozi mwandamizi wa CHADEMA akipanga mauaji ya mhariri wa gazeti.

“Mambo yako dhahiri, kwani video inaonesha pale ni nyumbani kwake. 

Pili, sikumtuma mtu akarekodi mkanda huo. Niliwahi kusema nina mkanda, haina maana kuwa nilituma mtu,” alisema.
Mwigulu aliongeza kuwa: “Mikanda niliyokuwa nayo nilipewa na kiongozi wa CHADEMA anayechukizwa na vitendo hivyo vya kinyama.

“Ndugu zangu wa CHADEMA, najua nawakera na hampendi kusikia haya, nawashauri msihangaikie habari ya Mwigulu ameshiriki, bali hangaikieni kwanini kiongozi mwandamizi anafanya hayo, pia kwanini anafanya kizembe mpaka mkanda unanaswa na tatu mjiulize,” alindika.

Ujumbe huo ulizidi kusomeka kuwa: “Kwangu mimi sioni kama kupata mkanda huo kwa kupewa au kwa hela ni dhambi kubwa kuliko ya kupanga mauaji. 

Niwambie tu mkanda niliopewa sikuweka hata nukta na nilikabidhi vyombo vya usalama,” alihitimisha.

Kufuatia ujumbe huo, wachangiaji mbalimbali waliujadili kwa njia ya mtandao huku wengine wakipiga simu katika chumba cha habari cha gazeti hili wakitaka Jeshi la Polisi litoe ufafanuzi ni kwanini limekaa kimya bila kumkamata na kumshtaki Mwigulu.

Mchangiaji mmoja katika mtandao huo, alisema: “Huo mkanda uliukabidhi lini kwa polisi? Mbona wao polisi wamefanyia kazi ule uliorushwa Jamii forums ?.

“Na je, kwanini utoke kipindi ambacho amefanyiwa ukatiri Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF), Absalom Kibanda miezi kadhaa mbele? Waweza kuni-convince (shawishi) kwamba si watu wa usalama wamefanya kitendo kile ili iendane vizuri na suala la Lwakatare?” alihoji.

Aliongeza kuwa: “Mwigulu kumbukeni huwezi ukafanya uchawi gizani miaka yote usigundulike, ipo siku Watanzania wataelewa ni fitna gani CCM mnazifanya.

“Suala la wauaji wa Kolimba (Horace) kuua, kwenda jela na baadaye kutolewa kinyemela lilitufunua fikra kidogo kuhusu Usalama wa Taifa na CCM, hili suala lilipita na likavumiliwa na Watanzania,” alisema mchangiaji huyo kwenye mtandao.

Kwamba hata suala la Dk. Stephen Ulimboka kupigiwa simu na mtu anayemfahamu, kuhojiwa na mtu huyo huyo baadaye kutekwa na kufanyiwa ukatili akiwa katika mazungumzo na mtu yule yule anayedaiwa kuwa alitumwa kutoka Ikulu bila kumkamata linatia shaka.

“Mtu aliyekuwa naye dakika za mwisho kwa maongezi alipaswa kukamatwa ili aisaidie polisi hata baada ya kutolewa mtiririko wa mawasiliano ya hawa watu wawili na gazeti la MwanaHalisi, hili suala pia lilitufunua mtazamo na fikra kuhusu CCM na Usalama wa Taifa.

“Na sasa hili suala la Lwakatare pia linatupa picha halisi ya CCM na Usalama wa Taifa, ila siwezi kubashiri kama litavumiliwa na kusahauliwa pia. Sifa ya kwamba Tanzania ni nchi ya amani inatolewa na watu wasiojua tafsiri halisi ya amani,” alisema.

Mchnagiaji mwingine katika mtandao huo alijadili utetezi wa Mwigulu akisema: “Huoni unajichanganya…imekuwaje unakuwa na mawasiliano na Ludovick (Joseph) na wakati huo huo unamtumia hela kwa M-pesa ?.

“Hii inaonyesha kuna kitu kimejificha, vyombo vya dola vimekaa na hiyo video miezi mitatu…ndipo mtuhumiwa akamatwe, huoni kuna walakini ?.

“Najua vyombo vya dola vilitaka kumteka Mhariri wa Mwananchi ila bahati mbaya watekaji wakaenda kwa Kibanda na video ikatolewa muda huo huo...huoni kwamba polisi inatakiwa kuhojiwa kwa kukaa na video miezi mitatu?” alihoji.

Mwingine aliandika akisema: “Unaweweseka we...wewe ni shahidi katika kesi hii...na ni engineer number moja wa mpango mzima...utaenda kujibu mahakamani.

“Kuja humu JF kujitetea ni kutafuta sympathy (huruma) toka kwa wafuasi wako....You have a big case to answer in the court of law.....get prepared...we mbunge gani unafanya ujasusi?” alihoji.

Aliongeza kuwa: “Unaacha kuwatumikia watu wako wanaokula majani jimboni mwako...unashiriki jinai. We kiongozi gani...maneno na matendo yako yanaonekana kwa Watanzania,” alisisitiza mchangiaji huyo.

Hata wachangiaji waliopiga simu walijikita kuhoji sababu za video kupelekwa kwa Mwigulu na kiongozi wa CHADEMA badala ya vyombo husika ili vichukue hatua.

Wapo waliohoji ni kwanini Mwigulu alitangaza kuwa na video ya mauaji kwenye vyombo vya habari wakati alikwisha wakabidhi polisi na wanaendelea na uchunguzi.

“Hapa kuna maswali mengi yanahitaji majibu na kama Jeshi la Polisi litafumba macho kuruhusu upuuzi huu wa siasa za kijinga kama hizi tutalipeleka taifa pabaya kwa michezo hii ya kina Mwigulu.

“Kitendo cha kutangaza kwenye vyombo vya habari wakati akijua polisi inaendelea na uchunguzi, kwanza angeweza kupoteza ushahidi, angeweza kudhuriwa lakini kwa muda wote zaidi ya miezi mitatu tangu akabidhi video hiyo mbona hakuna mauji yaliyotokea,” alisema Bakari Athuman mkazi wa Iringa.

Naye mwanaharakati aliyeomba kuhifadhiwa jina lake, alishangaa kuona polisi waliibuka kuifanyia kazi video hiyo baada ya Kibanda kuteswa, akihoji walikuwa wakingoja nini.

“Nadhani ukweli umeanza kujionesha kuwa huu ni mkakati wa kuichafua CHADEMA, maana Mwigulu anasema aliwapa video polisi, baada ya miezi mitatu wakawa kimya, kisha ikawekwa kwenye mtandaoo wa kijamii ndipo Lwakatare akakamatwa na kushtakiwa.

“Sasa tunajiuliza, ni nani aliweka video hiyo You tube kati ya Mwigulu na Jeshi la polisi? Je, kwani Mwigulu afahamu hata mahojiano baina ya polisi na Lwakatare? Kuna jambo limejificha, aibu yao inakuja,” alisema.

Katika mohojiano na gazeti hili kwa simu juzi, Mwigulu alikiri kuwa ndiye aliyeipeleka video ya Lwakatare polisi na kwamba alifanya hivyo baada ya kuripoti kuandikiwa ujumbe wa simu wa kutishiwa maisha na baadhi ya viongozi wa CHADEMA.

“Niliwapelekea mimi hiyo video polisi na wakati nasema kwenye televisheni nilikuwa tayari nimewapa. Na pale nilisema makusudi baada ya Zitto Kabwe kudai kuwa mwaka jana kulitokea mauaji mengi, ndipo nikataka kumuonesha kuwa chama chake kinahusika na mikakati hiyo,” alisema.

Alipoulizwa aliipataje video hiyo na kwanini hajahojiwa polisi ili kutoa uthibitisho wa uhalali wake, Mwigulu alisema: “Kuna msamaria mwema aliniletea.”

Mwigulu alipobanwa ana uhakika gani kama video hiyo ina ukweli, alijibu kuwa: “Ile huhitaji akili kubwa kutambua uhalisia wake.

Suala la Lwakatare CHADEMA wakubali tu na wajitokeze hadharani kwenye makanisa na misikiti, watubu na kuomba radhi kwa umma.”

Hata hivyo katika kile kinachoweza kuongeza mashaka ya Mwigulu  kuhusishwa kutengeneza video hiyo, alikwenda mbali zaidi akitoa hata siri za polisi, akisimulia maelezo aliyodai kuwa ndiyo yalitolewa na Lwakatare wakati akihojiwa na polisi.

“Pale video inaonesha ni nyumbani kwake, tena jikoni na hilo amekiri katika maelezo yake polisi. Pia amekubali kuwa siku hiyo alipiga chafya kama inavyoonekana. Sasa wewe mwandishi unatetea nini wakati yeye amekiri polisi kila kitu kilichomo mle,” alisema.

0 comments:

Post a Comment