.

.
Wednesday, May 22, 2013

10:24 AM

mwongela
MKUU wa wilaya ya Arusha , John Mongela amewataka vijana kujitambua na kujiamini huku wakiepukana na tabia ya kutumiwa na vyama mbalimbali vya siasa na kuishia kuwanufaisha wengine na wao kuendelea  kubakia maskini.

Aliyasema hayo jana  wakati akizungumza na vijana kutoka maeneo mbalimbali , ikiwemo vyuoni na wajasirimali wadogowadogo pamoja na viongozi  kutoka serikalini katika semina iliyofanyika mjini hapa .

Alisema kuwa, vijana wanapaswa kujitambua kuwa wana fursa mbalimbali ambazo wanapaswa kuzitambua na kuzitumia badala ya kubweteka na kukaa bila shughuli za kufanya na wengine kuishia kutumia na vyama mbalimbali vya siasa  hali inayochangia wengi wao kujiingiza katika makundi yasiyofaa.

 ‘unajua vijana wengi kutokana na kutokuwa na kazi za kufanya wameishia kutumiwa na vyama vya siasa hali inayochangia kwa kiasi kikubwa kuendelea kubaki kama walivyo na kuendelea kuwanufaisha vyama  hivyo, ni vizuri mjifunze kujituma na kutumia fursa zilizopo kwa kujiletea mafanikio zaidi’alisema Mongela.

Naye Mwenyekiti Mtendaji wa  chuo cha mafunzo ya uandishi wa habari na biashara (EABMTI) ,Rosemary Mwakitwange alisema kuwa, lengo la mkutano huo ni kuangalia namna ya vijana wa kitanzania wanaweza kupata fursa zilizopo hapa na kuweza kuzitumia kwa manufaa yao kwa ujumla.

Alisema kuwa, ili vijana waweze kujikwamua kiuchumi ni lazima tufike mahali sasa tuweze kuwajengea ujasiri wa kuweza kujitambua wao kwanza na hatimye kuzimbua fursa zilizopo katika maeneo yao na kuzitumia kwa manufaa yao na nchi kwa ujumla .

Alisema kuwa , chuo hicho ndio waratibu wa mradi huo hapa nchini  ambapo wamekuwa wakiandaa mikutano mbalimbali yanayohusiana na  maswala mbalimbali ya kiafya na kujamii ya vijana haswa wa kike wenye umri kati ya miaka 15 -24.

Aidha  mikutano hiyo wameshafanya  katika mikoa ya Pwani, Tanga, Iringa,Manyara,na Zanzibar ambapo hii ikiwa ni awamu ya pili  wamepanga kufanya mikutano mingine ya aina hiyo katika mikoa ya Rukwa, Kilimanjaro, Zanzibar,Mwanza,  na Ruvuma .

‘Unajua katika semina hii tunazungumzia  mradi wa ‘je tufanyeje  mradi unaodhaminiwa na shirika la USAID chini ya Sauti ya Amerika (VOA)  katika kujadili maswala mbalimbali ya vijana na fursa  za kiuchumi zilizopo miongoni mwao na kuweza kuzitumia kwa lengo la kuondokana na changamoto mbalimbali zinazowakabili na hatimaye kuwawezesha kufikia malengo yao’alisema Mwakitwange.

Aidha semina hiyo imedhanimiwa na shirika la misaada la watu wa Marekani (USAID) chini ya uangalizi na uandaaji  wa Idhaa ya Kiswahili ya sauti ya Amerika (VOA).

0 comments:

Post a Comment