.

.
Monday, May 20, 2013

8:59 AM
Na Bertha I. Mollel - Samunge, Loliondo

WANANCHI WAMLILIA TIBAIJUKA KUWEKA UPYA MIPAKA ILIKUEPUSHA VIFO NGORONGORO


Wananchi wa Kata ya Samunge kijiji cha Samunge Wilayani Ngorongoro mkoani hapa wamemuoamba Waziri wa Ardhi na maendeleo ya makazi,Profesa Anna Tibaijuka kurudi tena kijijni hapo na kuweka wazi mpaka  baina ya kijiji hicho na wafugaji kutoka Loita kwani mpaka alioweka bado una migogoro huku mgogoro huo ukiwa ni chanzo cha vifo vya wanyama na binadamu

Hayo yameelezwa na Kaimu Mwenyekiti wa Kijiji hicho Bw Wilson Mbande wakati akiongea na "majira"kijijini hapo  mapema juzi.

Aidha Bw Wilson alisema kuwa hapo awali waziri Tibaijuka aliweka mpaka katika eneo la kijiji cha Mudito na Maloni lakini sasa wafugaji wa kimasai wamekiuka amri hiyo na kudai kuwa wamepewa mpaka hadi mlima Samunge jambo ambalo sio la Kweli

Alidai kuwa Waziri alifika katika eneo hilo kwa ajili ya kusawazisha mgogoro baina ya makabila hayo mawili ambayo ni wasonjo na wamasai kutoka kenya lakini kwa sasa bado mgogoro unaendelea ni mkubwa sana 

Alifafanua kuwa hali hiyo si nzuri sana kwa kuwa watu wanapoteza maisha ovyo hasa katika nyakati hizi ambazo ni msimu wa kilimo hivyo eneo hilo la Samunge linapata matatizo makubwa sana 

"waziri alipokua alisema kuwa tayari mpaka umeshawekwa kwahivyo hatarajii kuona migogoro tena lakini alipoweka mpaka tu kabla hajafika arusha mjini hawa wenzetu walisema kuwa huu Mlima Samunge ambao upo kwenye eneo letu ni wao na kuanzia hapo watu na mifugo yetu inakufa ovyo hivyo tunamuomba Waziri Tibaijuka aje kwa mara nyingine tena aweze kuwaeleza na ikiwezekana kuweka mpaka wa wazi"alisema Wilson

Mbali na hayo alisema kuwa kutokana na wamasai hao kuvamia mlima huo ambao ndio tegemeo kubwa sana la wakazi wa Samunge hasa kwa shuguli za Kilimo na Ufugaji lakini pia wameathirika Kiuchumi kwani kwa sasa shuguli zote zimesimama 

Pia alisema kuwa hali hiyo inaendelea kuongeza umaskini mkubwa sana katika eneo hilo la Samunge hivyo basi Serikali inatakiwa kuhakikisha inaangalia mgogoro huo kwa undani sana kwani huwenda ukasababisha vifo vya watu wengi sana hasa kabila hilo la wasonjo watakapoanza kujichukulia sheria mkononi

"Ni Vema kama Serikali ikahakikisha kuwa inatatua suala hili ambalo ndani yake inaonekana kuna siasa za hali ya juu sana ili kuokoa maisha ya watu wengi ambao wanaweza kufa lakini pia hata uchumi wa eneo hili la Samunge nao utadidimia sana"alifafanua Wilson

0 comments:

Post a Comment