.

.
Tuesday, May 21, 2013

6:19 AM


Rais Jakaya Kikwete amemwagia sifa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa hatua ambayo inaweza kutafsiri mengi katika medani ya siasa nchini.
 
 Akizungumza na wabunge wa CCM kwenye Ukumbi wa White House Dodoma juzi, Rais Kikwete ambaye pia mwenyekiti wa chama hicho, alisema nguvu za Lowassa pekee zinatosha kushinda uchaguzi mdogo wa kiti cha udiwani Kata ya Makuyuni kilichoko wilayani Monduli.

Kata ya Makuyuni iko wilayani Monduli, ambako Lowassa amekuwa mbunge wake tangu mwaka 1995.

Habari za kutoka ndani ya kikao hicho zinaeleza kuwa Rais Kikwete alitoa kauli hiyo kuhusu kampeni za uchaguzi huo wa Makuyuni, baada ya kuwa ametoa ruksa kwa makada wa chama hicho wanaotaka urais kuanza kujipitisha pitisha miongoni mwa wanachama wa chama hicho. 

Lowassa anatajwa kuwa miongoni mwa wanaCCM wanaotaka kumrithi Rais Kikwete kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.

“Sina tatizo na pale Makuyuni, najua muscles (misuli) za Mzee Lowassa zinatosha kutupa ushindi; au vipi mzee?” alidokeza mmoja wa wabunge wa CCM akimnukuu Rais Kikwete.

Uchaguzi wa Udiwani Kata ya Makuyuni unaotarajiwa kufanyika Juni 16, mwaka huu, utakuwa wa ushindani mkali kati ya CCM na Chadema ambao historia yao kisiasa mkoani Arusha ni ya uhasama.

Katika uchaguzi huo, unaofanyika baada ya kifo cha Abdillah Warsama (CCM), chama hicho kitatetea nafasi yake kwa kumsimamisha Godluck Lerunya na Chadema ni Japhet Sironga. 

Mbali na Kata ya Makuyuni, uchaguzi wa udiwani mkoani Arusha utafanyika pia katika Kata za Kaloleni, Themi, Kimandolu na Elerai, kutokana na waliokuwa madiwani wa kata hizo (Chadema), kufukuzwa na chama chao.

“Mnaweza kuchafuana leo, kesho mkapata mgombea mwenye nundu nyingi na mabandeji kila mahala, halafu mkapata shida kumnadi,” alisema.
 
Siyo mara ya kwanza kwa Kikwete kumsifia Lowassa kwani aliwahi kufanya hivyo mwaka jana huko Longido wakati akikabidhi ng’ombe.
 
Pia aliwahi kumsifia wakati wa kampeni za uchaguzi za mwaka 2010 wakati Kikwete alipomwelezea Lowassa kama Mbunge makini na kuwaomba watu wa Monduli kumchagua tena.

Hata hivyo, alipoulizwa kama baada ya kuruhusiwa kuanza kujipitisha kwa wanaCCM kama anataka kuwania urais, Lowassa alijibu kupitia watu wake wa karibuni kuwa asingependa kuzungumzia suala hilo hasa baada ya Rais kutoa kauli hiyo.

Kutangaza nia ruksa

Rais Kikwete aliwaeleza wabunge hao kuwa si kosa kwa watu kutangaza nia ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ikiwamo urais mwaka 2015.

“Wabunge na mawaziri wenye nia ya kutangaza nia ya kugombea urais wawe huru, kwani hiyo ni haki yao, isipokuwa wafanye kwa wema bila kukivuruga chama na kuwagawa wanaCCM katika makundi. Sioni tatizo watu kujipitisha. Sisi sote hapa tulijipitisha. Lakini tufanye hivyo kistaarabu bila kuvurugana.”'

Aliwaagiza wabunge wa chama hicho kwenda majimboni mwao kusikiliza kero za wananchi badala ya kusubiri wakati wa uchaguzi.

Kauli ya Membe

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ambaye naye anatajwa kuwa miongoni mwa wagombea amewataka waandishi waache kuandika kila siku habari za urais na badala yake waandike mambo ya maendeleo. 


Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya kukutana na mabalozi wa nchi zinazoendelea kuhusu Mkutano wa Smart Partnership, unaotarajiwa kufanyika nchini, Membe alisema ni vizuri yakaandikwa mambo ya maendeleo na si kila wakati kuandika mambo ya urais.

“Mkutano kama huu nchi kama Kenya watauripoti vizuri na kwa undani hivyo mfanye hivyo si kila kitu urais 2015,” alisema Membe.

 Mkutano huo utaanza Mei 28, hadi Juni Mosi na utajadili jinsi gani sayansi na teknolojia vinaweza kutumika kuzikwamua kiuchumi.
chanzo:libeneke blog

0 comments:

Post a Comment