.

.
Monday, October 29, 2012

11:01 PM
LICHA ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kunyakua viti 22 kati ya 29 vya udiwani katika uchaguzi uliofanyika juzi, chama hicho tawala kimepoteza kata nne kilichokuwa kinazishikilia kabla ya uchaguzi huo.
Uchaguzi huo ulifanyika kuziba nafasi zilizoachwa wazi na madiwani walioondoka kutokana na sababu mbalimbali zikiwamo vifo.
Matokeo ya uchaguzi huo yanaonyesha kwamba katika Kata 29, Chadema wameshinda katika kata tano na kukifanya kuongeza madiwani watatu. TLP na CUF kila kimoja kimepata kata moja.
Kabla ya uchaguzi huo, Chadema kilikuwa na Kata mbili za Rombo na Mvomero ambazo kimefanikiwa kuzitetea na kuongeza nyingine tatu, ambazo ni Mlangila (Ludewa), Ipole (Tabora) na Daraja Mbili (Arusha) ambazo awali, zilikuwa zikishikiliwa na CCM.
TLP kilitetea kiti chake katika Kata ya Vunjo (Kilimanjaro) wakati CUF kilitwaa Kata ya Newala ambayo awali ilikuwa ikishikiliwa na CCM.
CCM kimetetea viti vyake vingine vilivyobaki ambavyo ni Msalato (Dodoma), Bang’ata (Arumeru Magharibi), Mletele (Songea), Mwawaza (Mjini Shinyanga), Lwezera (Geita), Bugarama (Kahama) na Bagamoyo mkoani  Pwani.
Viti vingine ni Mnero na Miembeni (Nachingwea), Myovizi (Mbozi), Mpapa (Momba), Mahenge (Ulanga), Vugiri (Korogwe), Tamota (Lushoto), Makata (Liwale), Mpepai (Mbinga), Kiloleli (Sikonge), Miyenze (Tabora), Karitu (Nzega), Lubili (Misungwi), Kilema Kusini (Moshi), Nanjara/Neha (Rombo), Lokokona (Nanyumbu) na Kitangiri (Newala).
Katika Kata ya Rwezera, Misango Jeremiah alishinda baada ya kupata kura 1,309 dhidi ya wapinzani wake, Ibuga Mussa (Chadema) aliyepata kura 933 na Mussa Mtagala (CUC) aliyepata kura 317.  Uchaguzi huo ulifanyika kujaza nafasi hiyo iliyokuwa wazi baada ya aliyekuwa Diwani wa Kata hiyo, Anatory Mkufu kufariki dunia kwa ajali ya gari Februari 23, mwaka huu.

Kilimanjaro
Katika Kata ya Kilema Kusini, Joseph Rubega wa TLP alishinda kwa kura 1,044 wakati Peter Temu (CCM) alipata kura 797 akifuatiwa na Serafine Mbuya (Chadema) kura 736 na Paul Shirima wa DP kura 13.
Katika Kata ya Nanjara Reheha, Rombo, Frank Salakana (Chadema) alishinda kwa kura 2,370 na kumshinda mpinzani  wake pekee kutoka CCM, Dismas Silayo aliyepata kura 1,128.

Lindi
Katika Kata ya Mnero Miembeni, Gervas
Ungele (CCM) alipata kura 818 wakati Jumanne Ali (CUF) alikuwa wa pili kwa kura 611 na Sinji Ali (Chadema) alipata kura 138.

Mbozi na Momba
Katika Kata ya Myovizi, Mbozi Cosmas Nzowa (CCM) alipata kura 1,726 huku Musa Mtakati  (Chadema) akipata kura 1,498.
Katika Kata ya Mpapa, Momba, Nolatico Simbeye (CCM) alishinda kwa kura 903 na mpinzani wake, Ladius Kasonso (Chadema) alipata kura 310.

Morogoro
CCM kilishinda katika Kata ya Mahenge kwa Mark Asenga, kupata kura 710 , dhidi ya Baltazar Kizee (Chadema) aliyepata kura 444.
Katika Kata ya Mtibwa, Mwakambaya  Edward (Chadema), alishinda kwa kura 3,096 na Musa Kingu (CCM) alipata kura 1,372.


Arusha
Kata ya Daraja Mbili, iliyokuwa ikishikiliwa na CCM kabla ya diwani wake, Bashiri Msangi kufariki dunia ghafla mapema mwaka huu, Chadema kiliibuka na ushindi baada ya mgombea wake, Prosper Msofe kupata kura 2,193 dhidi ya Philip Mushi wa CCM aliyepata kura 1,324. Mgombea wa CUF, Zani Hassan Zakaria alipata kura 162, William Msuyakura (TLP) alipata 42, Mohamed Msuya wa NCCR Mageuzi alipata kura 22.
Uchaguzi huo, unafanyika wakati bado kuna viti sita vya
udiwani katika Manispaa ya Arusha, vikiwa wazi. Madiwani watano kati yao walitimuliwa na Chadema na diwani mwingine wa Kata ya Sombetini, Alphonce Mawazo alijiondoa CCM na kujiunga na Chadema.

Nape alonga
Akizungumzia matokeo hayo jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema chama chake kinajivunia mafanikio yaliyopatikana katika uchaguzi huo mdogo akisema umeonyesha dalili kwamba wananchi bado wana matumaini nacho.
Alisema uchaguzi huo unaonyesha kuwa kinakubalika na wengi tofauti na inavyofikiriwa... “Tunajivunia ushindi katika Kata 22. Naweza kusema ni sawa na asilimia 75. TLP, ilipata kata moja na CUF kilipata kata moja na Chadema ilipata kata tano.”
Kutokana na ushindi huo, Nnauye aliendeleza malumbano yake na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa akimtaka achane na siasa badala yake awaachie vijana kukiendesha.
“Huu ni ushindi wa kimbunga, huo ni udiwani tu, pamoja na kwamba tumepoteza baadhi ya kata, lakini haisumbui sana kwani ushindi tuliopata ni wazi unaonyesha Chadema imepoteza mvuto kwa wananchi.
“Nawashukuru wananchi waliokiamini chama chetu na kukipa ridhaa ya kuongoza kata zao maana baadhi ya watu wamekuwa wakitoa taarifa za uongo kwamba kinaelekea kaburini lakini uchaguzi mdogo umewaonyesha walivyo waongo,” alisema Nnauye.
Alisema kinachomfanya amtake Dk Slaa kuachana na siasa ni kutokana na jitihada ambazo zimefanywa na chama hicho kuzunguka mikoa yote kikifanya kampeni za Vuguvugu la Mabadiliko (M4C) lakini akasema wameambulia patupu.

chanzo cha habari: mwananchi

0 comments:

Post a Comment