.

.
Monday, October 29, 2012

11:30 PM
Baada ya jeshi la polisi kutoa taarifa kwa waandishi wa habari juu ya kumtafuta Aliyekuwa Mbunge wa jimbo Arusha Mjini Godbless Lema, Mbunge huyo ashangwazwa na taarifa hizo alipoulizwa na kujibu taarifa hizo kwenye mkutano wa hadhara katika kata ya daraja mbili jijini Arusha.
Aliyekuwa mbunge wa jimbo la Arusha mjini Godbless Lema akihutubia mkutano wa hadhara kutoa shukrani kwa wananchi kwa kukichagua chama hicho  na kukanusha vikali madai yake ya kutafutwa na polisi

“Mimi nashangaa naletewa taarifa za kutafutwa na jeshi la polisi kwa tuhuma eti za kumpiga mtu na  kumjeruhi, saa ngapi na lini, mimi nina kazi tu ya kulinda kura siyo kupiga mtu kwani hata hao wanaojifanya ni wafuasi wa CCM ni kwamba hawajaelimika kuwa ukombozi unatakiwa hapa nchini hivyo siyo kuwapiga bali ni kuwaelimisha taratibu nao watabadilika tu.” Alisema Lema.

Aidha aliyasema hayo kwenye mkutano wa hadhara wa kutoa neno la shukrani kwa wananchi wa kata daraja mbili baada ya mgombea wao kushinda udiwani katika kata hiyo  Prosper Msofe(CHADEMA) octoba 28 kwa kuibuka kidedea kwa kura 2193 na kumuacha mpinzani wake wake wa karibu Philip Mushi(CCM) kwa kura  1324.
diwani teule wa kata ya daraja mbili Prosper Msofe(kushoto) akiwa na aliyekuwa mbunge wa jimbo la Arusha mjini Godbless Lema(kati) pamoja na mwenyekiti wa vijana chadema (BAVICHA), Ephata Nanyaro (kulia) wakijiandaa kutoa neno la shukrani katika kata ya daraja mbili

Katika mkutano huo Lema amewataka wananchi wa kata ya daraja mbili kumtumia diwani wao kuwaletea maendeleo ya kupata huduma za kijamii na siyo kumsumbua kwa kumpelekea shida ndogo ndogo za kuomba hela kwani haitawasaidia.

“Mtumieni diwani wenu kumsisitiza mara kwa mara kujenga barabara, kituo cha afya, kuleta maji, dampo au gari la taka n.k siyo kumgongea kila sikui kumuomba elfu moja kwani haisaidii kuliko maendeleo hiyo ni kumdidimiza diwani wenu ashindwe kuwasikiliza huku ni lazima wawasikilize na siyo ombi kwani ni mtumishi wenu na siyo bosi wenu”alisema Lema.

Hata hivyo Lema hakuishia hapo alimtupia diwani huyo teule madongo ya waziwazi, “Kwa sababu mmeshamchagua sasa ni mtumishi wenu na siyo bosi wenu hivyo lazima awasikilize ninyi muda na wakati wowote na akianza kuleta matambo na kupandisha mayenu au kutembea kisharobaro na kuvaa moka bila maendeleo yoyote tunampiga chini, tunamchagua mwingie” alisema Lema.


watoto nao waliwaleta watoto wenzao kusikiliza mkutano wa neno la shukrani kutoka kwa CHADEMA ingawa hawakupiga kura
Kwa upande wake diwani teule, Prosper Msofe kupitia chama hicho cha CHADEMA, aliwashukuru wananchi hao kwa kumwamini na kumchagua ambapo amewataka kutoa ushirikiano wao katika kuiletea kata hiyo maendeleo kama walivyoshirikiana katika kuhakikisha anashinda udiwani na kuwataka wananchi hao wamsindikize halmashauri siku anapokwenda kuapishwa ili kuonesha nguvu ya umma ipo kata ya daraja mbili pia.

0 comments:

Post a Comment