.

.
Friday, October 26, 2012

12:04 PM
vijana walioudhuria semina ya uraia na kutoa maoni ya katiba mpya inayotarajiwa kwenda kwa mkuu wa wilaya ya Arusha hivi karibuni ili kujihami endapo tume haitawapitia basi maoni yao yasibaki bali yawasilishwe na mkuu huyo
Imeelezwa kuwa uongozi usio na tija ni mzigo kwa watanzania ambao ni walipa kodi hivyo katiba ijayo ielekeze wizara zilizopo ili kuweka ukomo wa wiraza zinazoibuliwa kila siku bila tija wala manufaa kwa watanzania.

Hayo yamezungumzwa mkoani na Arusha na vijana wa kata ya daraja mbili na Lemara kwenye semina ya siku tatu ya Uraia iliyoandaliwa na Asasi isiyo ya kiserikali iitwayo Mategemeo Women Association(MWOA) na kuwezeshwa na Foundation for civil society.

Semina hiyo iliyowapatia vijana hao elimu ya uraia, wajibu na haki pamoja elimu ya katiba kwa ajili ya kujua kazi zake pamoja na katiba iliyopo kwa ajili ya kutoa maoni yao walipewa nafasi ya kutoa maoni yao ambapo walisema kuwa kuwepo kwa wizara nyingi serikalini ni mzigo usio na tija kwa walipa kodi(Watanzania).

Waliongeza kuwa kutokana na hayo wanaomba katiba ijayo ipunguze mzigo huo kwa kuweka ukomo wa wizara serikalini zinazojulikana tena zenye tija kwa watanzania na taifa kwa ujumla kuliko kila kiongozi akiingia madarakani kubuni wizara yake na kuweka watu wake hata wasio na sifa wala taaluma.

Mbali na hilo Waliongeza kuwa katiba ijayo iweke wazi madaraka ya viongozi wetu kwa kutoruhusu mtu mmoja kushika nyadhfa nyingi kwa wakati mmoja ikiwemo mbunge kutoruhusiwa kuwa waziri kwani kufanya hivyo ni kuwanyima watanzania wengine nafasi za ajira na kuwanyima haki wananchi waliomchagua kuwawakilisha(kuwasemea bungeni) badala yake anakuwa anaisemea serikali na kuwasahau wananchi.

Aidha katiba ijayo pia  ielekeze namna ya kumuondoa madarakani kiongozi anayechaguliwa na wananchi anaposhindwa kazi ya kiutekelezaji na kuwa kiongozi mbovu kwa kuhamasisha maswala ya rushwa, uvunjifu wa amani, uhalifu n.k na kumchagua mwingine ili kuwaondoa viongozi watakaokuwa wabadhirifu wa fedha za umma na wazembe katika kuwatumikia wananchi.

Mmoja wa vijana hao Ally Manyanya alisema kuwa pia Rais apunguziwe madaraka ikiwemo uteuzi wa baadhi ya watendaji wa umma kama TAKUKURU na tume ya uchaguzi kwani hujikuta wakifanya kazi chini ya rais na chama chake hivyo wamependekeza kuwa watendaji hao wapitishwe na bunge sambamba na Rais kuteua mawaziri kulingana na taaluma zao ili kutenda kazi kwa ufanisi zaidi.

Manyanya aliongeza kuwa mbali na hayo pia katiba ijayo iamue na kuelekeza au kufafanua muundo wa serikali ya muungano kwani kwa sasa Tanganyika Tunajiita Wanzania huku Wazanzibar wakibaki na jina lao na kuwa na serikali yao, katiba na bunge hivyo katiba ielekeze muungano huu kama muungano kuwe na serikali moja ua Tanganyika wawe na serikali yao na Zanzibar serikali yao huku wakiwa chini ya serikali nyingine ya tatu ya Jamhuri.

Kwa upande wake Shaban Willium alipendekeza katiba ijayo iondoe kikwazo cha ajira kwa vijana ikiwemo kuajiriwa bila kuzingatiwa uzoefu wake bali taaluma yake, pia  viongozi wa serikali kuanzia ngazi za chini akiwemo balozi wa nyumba kumi, mwenyekiti n.k walipwe posho ili kupunguza upmbaji na upokeaji wa rushwa kwao pia uongozi wa balozi usitokane na chama tawala bali mfumo wa vyama vingi kama mwenyekiti.

Aliongeza kuwa katiba ijayo pia ieleze mfumo maalum wa elim kuliko kila kiongozi kuingia na mfumo wake pia Mila, Tamaduni na Desturi ziwe na mipaka ya kutovunja sheria za nchi kwa kigezo cha mila, desturi na utamaduni, ambapo pia alipendekeza adhabu ya kifo kuondolewa kwani adhabu hiyo inakiuka haki za binadamu ya “kila mtu ana haki yan kuishi”.

Naye mwenyekiti wa Asasi hiyo ya MWOA, Bi, Agness Saibulu alisema kuwa semina hiyo ya siku tatu iliyowashirikisha vijana 30 kutoka katika mitaa ya kata za daraja mbili na lemera wamefanikiwa kujifunza historia fupi ya Tanzaniia, elimu ya uraia, haki na wajibu wa kijana katika kushiriki mambo ya maendeleo ikiwemo vikao vya kiserikali, upigaji kura n.k pamoja na katiba, demokrasia, uongozi na uchumi ambapo pia wametoa maoni yao ya katiba mpya na kuipeleka kwa mkuu wa wilaya kuiwasilisha endapo tume haitawafikia.
kushoto ni mratibu wa semina hiyo ya uraia, Violla Ndikindikoki akiwa na mwenyekiti wa Asasi ya MWOA, Agness Saibulu (wa katikati), anayefuata ni mmoja wa wakufunzi wa semina hiyo Isaya Doita(kulia) ambaye pia ni diwani wa kata ya ngarenaro jijini Arusha wakijadiliana jambo.

0 comments:

Post a Comment