.

.
Thursday, November 8, 2012

8:46 PM

Wafanyakazi wa kiwanda cha kutengeneza vyandarua na t.shirt cha ATOZ cha Jijini Arusha wamedai kuwa uongozi wa kiwanda hicho umemudanganya Rais Dkt Jakaya Kikwete kuwa wafanyakazi wa kiwanda hicho wanalipwa maslahi mazuri.
 
Rais Kikwete wiki iliyopita katika ziara yake Mkoani Arusha alifanikiwa kukitembelea kiwanda hicho na kituo cha utafiti kilichopo kiwandani hapo na ujionea shughuli mbalimbali za maendeleo zinazofanywa na wafanyakazi hao.

Wafanyakazi zaidi ya 10 wakiongea na waandishi wa habari walisema kuwa ni baadhi ya wafanyakazi wa idara ya kutengeneza mifuko ya sembeti na ya kawaida ndio wanalipwa vizuri kwa kiasi cha shilingi 180,000 ukiondoa makato.

Mfanyakazi huyo ambaye aliomba kutotajwa jina lake alisema idara zingine hulipwa mshahara wa fedha raslimu shilingi 105,000 baada ya makato kwani kwenye karatasi za malipo {par roll} huonyesha shilingi 130,000 tu.

Alisema mbali ya hilo mfanyakazi anayeumia kazini kama vile kukatwa mkono na mashine na kupata ajali kazini mfanyakazi hukopeshwa fedha na uongozi wa kiwanda ili apate matibabu na baadae hukatwa katika mshahara wake.

‘’Sasa tumeambiwa tuimbe nyimbo za kumsifu Rais na kuusifu uongozi wa kiwanda kwa kulipwa vizuri mbele ya Rais wakati sio kweli huku ni kumdanganya Rais ‘’alisema

Mfanyakazi mwingine ambaye pia aliomba asitajwe  alisema uongozi wa kiwanda haulipi malipo ya kazi ya ziada{over time},haulipi malipo ya kodi ya pango na umekuwa ukiwanyanyasa wafanyakazi kama enzi za utawala wa makaburu nchini Afrika ya kusini.

‘’tunawaomba nyie waandishi wa habari andikeni ukweli juu ya kiwanda hiki cha A TO Z kwani kuna mambo makubwa sana uongozi wa serikali unapaswa kuyajua na kuyafanyia kazi lakini mkikaa kimya mtawaangamiza mamia ya watanzania wenzenu waliopo pale kwa kasababu tu ya umaskini’’alisema mfanyakazi huyo.

Alisema mfanyakazi anachukuliwa majira ya saa 12 asubuhi kuingia kazini na bus la kampuni na kurudishwa saa 1.30 usiku,mfanyakazi anafanya kazi kama punda zaidi ya masaa 12 tofauti na kawaida ya mfanyakazi kufanya kazi masaa 8 tu.

Akizungumzia hilo Mkurugenzi Mtendaji msaidizi wa kiwanda cha ATOZ ,Godwini Abeid alipinga na kusema kuwa madai yaliyotolewa na wafanyakazi hao hayana ukweli hata mmoja na kueleza kuwa ni uzushi uliotungwa.

Abeid alisema mbali ya kuajiri mamia ya wafanyakazi katika kiwanda hicho alisema hakuna mfanyakazi anayelipwa kiwango cha mshahara wa serikali cha shilingi 80,000 kwani wafanyakazi wote wanalipwa juu ya kiasi hicho.
Alisema suala la mfanyakazi kukatika mkono ama kuumia akiwa kazini kiwanda ndio kinagharamia matibabu yote na hakuna mfanyakazi aliyekatwa mshahara kwa ajili kufidia matibabu yaliyolpwa na uongozi wa kiwanda.

‘’hapa kila kitu kipo sawa na tunalipa vizuri misharahara na masaa ya ziada na kama kuna wafanyakazi wamekuja kulalamika na kusema uongozi umemdanganya Rais sio kweli bali wao ndio wamewadanganya nyie ‘’alisema

Naye Mwenyekiti wa chama cha wafanyakazi wa viwandani{TUICO} Rehema Abdallah alisema kuwa yeye kama mtetezi wa haki za wafanyakazi kwa kushirikiana na kamati yake wako mstari wa mbele kuhakikisha maslahi ya wafanyakazi wa kiwanda hicho wanalipwa vizuri .
   
chanzo na libeneke blog
 

0 comments:

Post a Comment